Tanzania kuomba kuwa mwenyeji wa Mashindano ya AFCON mwaka 2027

NA DIRAMAKINI

RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan kwa kushirikiana na Kenya na Uganda kupitia Pamoja Bid wamedhamiria kuwa mwenyeji wa michuano ya Fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika (African Cup of Nations) 2027.

Rais Samia amesema nchi hizo zinawania nafasi hiyo kwa kutambua mafanikio makubwa ambayo Sekta ya Michezo imepata, hivyo kuwa wenyeji wa AFCON 2027 kutaongeza hamasa zaidi kwa ukuaji wa michezo hususan soka.

Aidha, Rais Samia amesema michuano hii itachangia katika ukuaji wa utalii kwa kuwa ni mashindano ambayo hutazamwa na zaidi ya watu bilioni moja Barani Afrika na maeneo mengi duniani kwa ujumla.

Vile vile, Rais Samia amesema mashindano hayo yataleta watu mashuhuri nchini wenye ushawishi duniani hivyo huwezesha na kunufaisha sekta nyingi za uchumi ambapo huchangia ajira, mapato kwa wafanyabiashara na serikali.

Kwa upande mwingine Rais Samia amesema Serikali kupitia Wizara ya Utamaduni Sanaa na Michezo kwa kushirikiana na Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania, imeshafanya utafiti na kuandaa mpango mkakati wa utekelezaji wa maandalizi ya kuwa mwenyeji wa mashindano hayo.

Mashindano ya AFCON yataweka rekodi kwa mara ya kwanza kufanyika katika Ukanda wa Afrika Mashariki tangu yalipoanzishwa rasmi mwaka 1957.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news