TANZANIA,BORA KUISHANGILIA-17: Hii ndiyo Mwanza,Pia ni zaidi ya uijuavyo

NA LWAGA MWAMBANDE

HISTORIA inaonesha kuwa,Mkoa wa Mwanza ulianza wakati ukiwa chini ya tawala za kitemi za Wasukuma, Wazinza, Walongo, Wakara na Wakerewe kabla ya ukoloni.

Picha na MITU.

Wajerumani walipotawala Tanganyika eneo la Mwanza likawa mojawapo ya wilaya katika himaya ya utawala wa Kijerumani.

Utawala wa kikoloni wa Mwingereza ulipokabidhiwa uangalizi wa Koloni la Afrika Mashariki baada ya vita kuu ya Dunia, ulianzisha utawala wa majimbo yaani Provinces. Tanganyika ilikuwa na majimbo ya kiutawala nane na mojawapo likiwa ni Lake Province.

Lake Province liliundwa kwa kujumuisha maeneo ya wilaya za Mwanza, Biharamulo, Bukoba, Maswa, Shinyanga, Musoma na Kwimba.

Baadaye Lake Province liligawanywa na kuunda majimbo mawili la Lake Province (Sukuma Land) na Western Province). Utawala wa Mwingereza ulimalizika na Tanganyika kupata uhuru mwaka 1961.

Aidha,baada ya uhuru Mwanza iliendelea kuwa sehemu ya Jimbo la Lake Province chini ya mtawala wake kwanza wa jimbo (Provincial Commissioner) aliyeitwa Provincial Commissioner Bw. Walden, ambaye alikabidhi madaraka kwa Richard Wambura.

Mkoa wa Mwanza ulianzishwa rasmi mwaka 1963 ukiwa na wilaya nne za Ukerewe, Geita, Mwanza na Kwimba. Mwaka 1972 baada ya sera ya madaraka mikoani wilaya zaidi zilianzishwa kwa kuanza na Magu mwaka 1974. Wilaya ya Sengerema ilianzishwa mwaka 1975 ambapo awali ilikuwa ni tarafa mojawapo ya Wilaya ya Geita.

Misungwi ilianzishwa mwaka 1995 ambapo awali ilikuwa ni eneo la tarafa za wilaya ya Kwimba, Ilemela na Nyamagana zilianzishwa mwaka 2002 ambazo zilikuwa zinaunda wilaya ya Mwanza.

Mwaka 2010 mikoa mipya ya Geita na Simiyu ilitangazwa kuanzishwa. Wilaya mpya pia za Busega na Nyanghwale nazo zilitangazwa kuanzishwa 2010 na utekelezaji wake utaanza rasmi wakati wowote katika mwaka wa fedha 2011/12.

Mkoa wa Mwanza ni kati ya mikoa 26 ya Tanzania Bara na mikoa 31 ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.Mkoa wa Mwanza unapakana na Geita upande wa Magharibi, Shinyanga na Simiyu upande wa Kusini na Mara upande wa Mashariki. Ziwa la Viktoria liko Kaskazini.

Makabila makubwa katika Mwanza ni Wasukuma kwa wilaya za Sengerema, Magu, Kwimba, Misungwi na Ilemela huku ilaya ya Nyamagana wanaishi makabila tofauti tofauti na Wilaya ya Ukerewe hupatikana Wakerewe na Wakara. Mshairi wa kisasa, Lwaga Mwambande anasema, karibu jijini Mwanza, jiji la miamba. Endelea;

1. Mwanza huko ntarudia,
Remmy tulimsikia,
Wafaa kuusifia,
Ni mengi umesheheni.

2. Kwa uchumi kuchangia,
Ni wa pili Tanzania,
Kodi nyingi wachangia,
Maendeleo nchini.

3. Wanajituma kwa nia,
Nyanja zote watimia,
Kilimo mifugo pia,
Hizo ni za kwao fani.

4. Viwanda samaki pia,
Mwanza naishangilia,
Minofu twajiuzia,
Kwetu fedha za kigeni.

5. Ninavyowafagilia,
Ukarimu wazidia,
Ugali kikupatia,
Utashiba kama nini.

6. Na Ziwa Victoria,
Kiuchumi lachangia,
Wavuvi wajipatia,
Pesa tele mifukoni.

7. Tena ukiangalia,
Kazi wanajifanyia,
Kutegea kusikia,
Kwao hiyo asilani.

8. Pesa wakijipatia,
Zile wamejivunia,
Wanajua kutumia,
Kujiletea amani.

9. Jasho kama lakujia,
Kazi unajifanyia,
Vizuri kufurahia,
Jasho lako kwa amani.

10. Barabara Mwanza pia,
Jiji kweli lavutia,
Rock City kisikia,
Mji wa kando ziwani.

11. Usiku kizungukia,
Daraja juu sikia,
Taa tamu angalia,
Mwanza utaitamani.

12. Supu ya samaki pia,
Waweza kujipatia,
Vyakula vimejazia,
Mwanza mi niseme nini?

13. Madini dhahabu pia,
Huko Mwanza yajazia,
Utalii fwatilia,
Saanane kisiwani.

14. Jiji la mawe tambia,
Watu wanajiishia,
Kama wawafwatilia,
Utaishia njiani.

15. Visiwa vingi sikia,
Twajaliwa Tanzania,
Ukerewe kisikia,
Ndicho kikubwa amini.

16. Kisiwa twajivunia,
Watu ilotupatia,
Mengi wametufanyia,
Nchini na Duniani.

17. Mmoja nakutajia,
Jina mnalijulia,
Beijing tingishia,
Akawika duniani.

18. Mama Mongella sikia,
Sisi tunajivunia,
Mengi ametufanyia,
Nchini na duniani.

19. Beijing kuanzia,
Kongamano kukalia,
Wanawake nakwambia,
Alitamba duniani.

20. Na hapo hakuishia,
Makubwa litufanyia,
Kiti alishikilia,
Spika Bunge Barani.

21. Afrika nakwambia,
Spika Mtanzania,
Wa kwanza ninakwambia,
Sifa zikaja nchini.

22. Kule alikoanzia,
Ni Ukerewe sikia,
Huko wanajivunia,
Ufugaji si madini.

23. Ukiweza kufikia,
Kweli utafurahia,
Fukwe zinazovutia,
Kwa upepo wa jioni.

24. Ninakuhakikishia,
Huwezi ukajutia,
Boti za kusafiria,
Ziko zaidi ya teni.

25. Watu wa huko sikia,
Akili zawazidia,
Samaki ukijilia,
Eti akili kichwani

26. Ya moyoni kukwambia,
Waziwazi wakwambia,
Wako huru kisikia,
Mambo yote hadharani.

27. Magu Mwanza angalia,
Mtu aliibukia,
Kuibeba Tanzania,
Jumuiya ya Kusini.

28. Huyu ninakutajia,
Daktari katimia,
SADC lishikilia,
Ule wenyewe mpini.

29. Huyo ninakutajia,
Stargomena sikia,
Kweli twamfagilia,
Alofanya ugenini.

30. Maarufu nakwambia,
Huko alikopitia,
Kazi alitufanyia,
Miaka nane kitini.

31. Daktari wetu pia,
Kitu katuanzishia,
Andika historia,
Ya kukumbukwa nchini.

32. Tangu huru Tanzania,
Miaka unosikia,
Hutukuwahi sikia,
Waziri huyu nchini.

33. Mwanamke kuingia,
Waziri alotimia,
Ulinzi kwangu sikia,
Ni wa kwanza wizarani.

34. Mtendaji katimia,
Nchi inajivunia,
Mambo ya nje sikia,
Kwa sasa yuko kitini.

35. Uhuru kupigania,
Ushirika shikilia,
Nani hajamsikia,
Mkuu Paul Bomani?

36. Nchi alitumikia,
Hadi alipoishia,
Vizuri kumsifia,
Hatunaye duniani.

37. Jinsi alivyochangia,
Ushirika nakwambia,
Kwa kweli tulitambia,
Enzi za kale nchini.

38. Sasa ukiangalia,
Nani anamfikia,
Ushirika wasikia,
Watambatamba nchini?

39. Changamoto nakwambia,
Wezi walipoingia,
Kwa sana ukafifia,
Sasa kama u wodini.

40. Tufanye kufwatilia,
Pale walipoishia,
Waliotutangulia,
Upae tena nchini.

41. Ushirika nakwambia,
Kama wajishikilia,
Hata wanachama pia,
Wanakuwa na Amani.

42. Mazao kijiuzia,
Pesa wanajipatia,
Yao wanajifanyia,
Kwa furaha na Amani.

43. Kusiwe kulialia,
Mtu kulalamikia,
Ya kwamba kawaibia,
Kutaka atiwe ndani.

Lwaga Mwambande (KiMPAB)
lwagha@gmail.com 0767223602

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news