Wafanyabiashara Kariakoo wakubali yaishe, wasitisha mgomo

NA DIRAMAKINI

BAADA ya wafanyabiashara wa Soko Kuu la Kariakoo kupanga kufanya mgomo wa kufunga maduka kushinikiza Serikali kutatua kero zao, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, CPA Amos Makalla mapema leo amekutana na wafanyabiashara hao na kufanikiwa kumaliza mgomo huo.

Akitoa tamko la Serikali,CPA Makalla amesema Serikali imewaelekeza Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) kusitisha Operesheni ya Kamatakamata mpaka pale ufumbuzi wa pamoja utakapopatikana.

CPA Makalla amesema hivi karibuni Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Kassim Majaliwa atafanya kikao na Kamati ya Wafanyabiashara wa Kariakoo katika Ofisi ya Waziri Mkuu Magogoni jijini Dar es Salaam ili kupata suluhu ya pamoja katika kumaliza tatizo hilo ambapo kwenye kikao hicho kitajumuisha pia mawaziri wa kisekta.

Pamoja na hayo,CPA Makalla ametoa wito kwa wafanyabiashara hao kuendelea kufanya biashara kwa amani na utulivu wakati Serikali ikiendelea kufanyia kazi madai yao huku akihimiza kulipa kodi kwa mujibu wa sheria.

Baada kukamilika kwa kikao hicho cha maridhiano,wafanyabiashara wote walielekea kwenye maduka yao na kuyafungua ambapo baadhi ya wafanyabiashara wamemshukuru Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan kwa kusikiliza na kutatua kero yao kwa wakati na wameahidi kushirikiana na Serikali.

Awali, wafanyabiashara hao walimweleza Mkuu wa Mkoa kuwa, wamechoshwa na mfumo uliopo wa ulipaji kodi, kwani ipo tofauti na nchi nyingine hivyo wateja wao wamewakimbia kutokana na kukamatwa na mizigo yao na huku wengine mizigo yao ikishikiliwa mpaka leo.

Hivyo wanamuomba Rais Dkt.Samia afike ili awasikilize kwani siku za nyuma walishaenda viongozi mbalimbali lakini hakuna kinachoendelea huku wao wakiendelea kuumia .

"Kwa kweli soko hili wafanyabiashara tumekuwa wazalendo kwa kuvumilia mengi na kila tunapopeleka malalamiko yetu hayafanyiwi kazi, hivyo kupitia mgomo huu tulioamua tufunge maduka yetu mpaka Rais atakapoamua kuja na tukaa naye meza moja kuzungumza na kutusaidia kusuluhisha mgogoro ambao umedumu kwa muda mrefu,"amesema Benard.

Mwenyekiti wa Jumiuya wa Shirikisho wa Wafanyabiashara Tanzania, Martin Mbwana amesema, wamekuwa wakikutana na viongozi mbalimbali, lakini wakishatoa maagizo kuzuia operesheni ya watu wa TRA wakishaondoka huku nyuma maagizo yao hayatekelezwi na TRA wanakuja juu na kusema utaratibu uko palepale na kilichoongelewa kinabakia ni siasa, hivyo wanaomba jambo hilo liangaliwe kwa jicho la tatu na serikali.

Naye Mwenyekiti wa Vituo vyote vya Wafanyabiashara Kariakoo, Rwaimamu Erasto amesema, inawaumiza sana mrundikano wa kodi yao mzigo yao kila inapopita wakiagiza kutoka nje ya nchi wanalipishwa kodi wakileta dukani wanalipia kodi, bado wanalipia pango, bado wanaambiwa kuna sheria ya kodi ya stoo wakiwauzia wateja nao wanakamatwa kudaiwa kodi, "kiukweli ni shida hivyo wateja wametukimbia na kwenda masoko mengine".

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news