Aagizwa kumlipa Mkandarasi wilayani Manyoni

NA DIRAMAKINI

SIKU chache baada ya Katibu Tawala Mkoa wa Singida, Dkt. Fatma Mganga kutoa maagizo kwa Mkandarasi anayejenga wodi mbili na nyumba ya kuhifadhia maiti wilayani Manyoni ya kuwalipa staahiki zao mafundi na vibarua, Juni Mosi, Mkuu wa Mkoa huo, Peter Serukamba naye ametembelea eneo hilo na kumuagiza Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manyoni kulipa fedha za Mkandarasi huyo na kuwalipa mafundi pamoja na vibarua ili kazi iweze kukamilika kwa wakati.
RC Serukamba ametoa maagizo hayo baada ya kupewa taarifa na Mhandisi wa wilaya hiyo, Gabriel Mayaya kwamba, kazi ya ujenzi inachelewa kwa sababu Mkandarasi haonekani eneo la kazi na vibarua hawajalipwa fedha zao jambo ambalo huchangia kusuasua kwa kazi hiyo ndipo alipotoa maelekezo fedha hizo kukatwa na kuwalipa vibarua na mafundi huku akimtaka Mhandisi huyo kuongeza usimamizi ili kazi ikamilike kwa wakati.

"Huwezi kuacha kuwalipa vibarua halafu utegemee kazi itamalizika, Mhandisi kaa na Mkurungezi chukueni fedha za Mkandarasi lipeni vibarua wake kwa kuwa inafahamika kiasi wanacholipwa kwa kazi walizofanya,"amesema Serukamba.

Aidha, amemuagiza Mhandisi Mayaya kuongeza mafundi wengine kwa kuwa sehemu ya ujenzi iliyobaki ni kubwa na mafundi ni wachache huku muda ukiwa ni mdogo uliobaki.

"Hatuwezi kumsubiri mtu ambaye hata ‘site’ haonekani, fedha zake walipeni hao vibarua na tafuteni mafundi wengine ili kazi ikamilike kwa wakati."

Hata hivyo RC Serukamba amebainisha kwamba mtumishi yeyote atakayeshindwa kusimamia miradi ya maendeleo Mkoani Singida na akasababisha fedha kurudi hazina watakuwa wamehatarisha vibarua vyao.

Hata hivyo akiongea kwa niaba ya Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manyoni, Elias Moleli (Afisa Maendeleo ya Jamii) wilayani hapo amemuahidi Mkuu wa Mkoa kwamba wataongeza mafundi na watahakikisha kazi inafanyika usiku na mchana na kwa viwango vinavyotakiwa.

Aidha, Moleli amesema tayari wamenunua vifaa vyote muhimu vikiwemo mabati nondo na madirisha na mbao kwa ajili kukamilisha kazi hiyo.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news