Malya kuboresha miundombinu ya michezo

NA ADELADIUS MAKWEGA

MKUU wa Chuo cha Maendeleo ya Michezo Malya, ndugu Richard Mganga amesema kuwa maendeleo ya chuo anachokiongoza yanakwenda kwa kasi huku miradi kadhaa ya maendeleo ikielekezwa na serikali kwa miaka kadhaa mfululizo chuoni hapa. 
Hayo yamesemwa Mei 31, 2023 katika kikao cha kawaida na wakufunzi wanaosoma chuoni hapa katika kozi mbalimbali za michezo Uwanja wa Ndani uliyopo Malya Kwimba mkoani Mwanza. 

“Kuna wakati tulikuwa tunapokea wanachuo 40 tu, kwa kozi mbalimbali lakini kwa sasa tuna makundi ya mamia, wakati huo tulikuwa tukipokea hao arobaini, tulikuwa hatupokei tena hadi wanachuo hao wahitimu ndipo tuanze tena kudahili upya, sasa umati huu ni ushahidi kuwa udahili umeongezeka. Shabaha yetu ni kuongeza udahili wetu na ndiyo maana kumekuwa na uboreshaji wa mabweni na majengo mengine hatua kwa hatua, mfululizo.” 
Akiendelea kuongea katika kikao hicho huku makofi yakitawala aliwaomba wanachuo hao kutilia maanani mafunzo yao, akibainisha namna serikali inavyofuatilia chuo hiki kwa ukaribu mkubwa. 

“Nawaambieni kuwa tunatarajia ujio wa Mwenge wa uhuru ambao utaweka jiwe la msingi katika mradi wa ghorofa tatu wa bweni, huku viongozi wa Kiserikali wanatarajiwa kufika kuona maendeleo ya chuo chetu.” 
Wakizungumza mara baada ya Mkuu wa Chuo Mganga kuongea, wanachuo hao kwa pamoja wamepongeza serikali kwa maboresho hayo huku wakiomba juhudi zaidi katika kuinua michezo hapa nchini hususani katika ujenzi wa miundo mbinu ya viwanja kadhaa nchi nzima. 

“Kwa hakika tunapata mafunzo mazuri lakini hali ya miundo mbinu mashuleni si nzuri, hilo linahitaji maboresho makubwa ili jamii ya Watanzania waweze kushiriki michezo kikamilifu.Matarajio yetu sisi tukihitimu hapa tunalo jukumu pia la kwenda kuboresha miundo mbinu hiyo kupitia wadau.” 
Hayo yalisemwa na Baptist Kapinga ambaye ndiye Mwenyekiti wa Serikali na Rais wa Wanachuo. 
Kikao hicho kilihitimishwa kwa wanachuo hao kuzungumza na Mwadili wao mkufunzi Epifania Mugaga kwa faragha.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news