NA FRESHA KINASA
NAIBU Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Butiama mkoani Mara, Mheshimiwa Jumanne Sagini amesema kuwa Chuo Kikuu cha Kilimo na Teknolojia cha Mwalimu Julius K. Nyerere (MJNUAT) kilichopo wilayani Butiama kitaanza kutoa mafunzo ndani ya mwaka huu.
Mheshimiwa Sagini ameyasema hayo leo Juni 25, 2023 aliposhiriki ibada takatifu katika Kanisa la Parokia teule ya Mtakatifu Paulo V1 Jimbo la Musoma lililopo Nyabange Wilaya ya Butiama mkoani humo. Ambapo ameshiriki harambee ya ujenzi wa Kanisa hilo. Akiwa ameongozana na madiwani pamoja na viongozi mbalimbali kutoka katika Jimbo la Butiama.
Mheshimiwa Sagini ametoa shukrani za dhati kwa Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kufanikisha taratibu za kuanza lwa chuo hicho kwani kilikuwa ni kitendawili na ni miaka 12.
Hivyo, amewahimiza wananchi wa wilayani ya Butiama kutumia fursa ya uwepo wa chuo hicho kuanzisha miradi ya huduma muhimu itayowasaidia kujikwamua kiuchumi.

Amesema, Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Dkt.Samia Suluhu Hassan imekusudia kuanzisha na kukamilisha miradi ya maendeleo kwa kila sekta ikiwemo na Wilaya ya Butiama ambayo imepewa kipaumbale katika miradi ya afya,elimu,maji na barabara.
"Hivyo, niwaombe wananchi wa Butiama muendelee kuwa na imani na Serikali kwa kipindi kilichosalia tutazidi kutekeleza mengi na mazuri. Tuzidi kumuombea Rais wetu, viongozi wetu na tushirikiane kwa pamoja kuijenga nchi yetu,"amesema Mheshimiwa Sagini.