SIMULIZI YA KUTISHA KATIKA MAISHA-32

NA WILLIAM BOMBOM

Ilipoishia...mwili wa mtoto THE BOMBOM uliendelea kung'ara kwa muda wa dakika tano kisha ukarudi katika hali ya kawaida.

Wale wachawi wakabaki wakisema "hakika huyu ni mwana wa mungu" wakapiga kelele juu ya mlima Makamelwa wakilitukuza jina la mungu wao kisha wakarudi kambini kwao.

Endelea...

Walifika kambini muda wa saa tisa kasoro, wakapanga mipango ya namna ya kukutana usiku huo kwa ajili ya kwenda kuzindika eneo la kanisa.

Wachawi hao kwa pamoja walikubaliana kuweka zindiko kuu ndani ya eneo la ujenzi wa kanisa katika hatua zote yaani kabla ya ujenzi, wakati wa ujenzi na baada ya ujenzi. Baada ya hapo kila mmoja aliondoka na kurudi makwao.

Kwa upande wa mtoto THE BOMBOM alikuwa na muda mrefu hajarudi nyumbani kwao, aliamua alfajiri hiyo kurudi nyumbani ili aonane na babu yake kipenzi.

Ni zaidi ya majuma mawili hakuwepo nyumbani akizurura huku na huku akifanya miujiza. Babu yake akawa anasikia miujiza aliyokuwa akiifanya mjukuu wake kupitia wambea waliokuwa wakimfikishia taarifa.

Alichukua ungo kambini hapo kisha akaupanda, safari ya kuelekea Ilongo ikaanza. Kulingana na uzoefu wake wa kuendesha vyombo hivyo, alitumia muda muchache kufika nyumbani kwao.

Alikwenda kushuka nyuma ya nyumbani kwao, pembeni kidogo mwa mti mkubwa wa mwembe. Aliuchukua ungo huo akauhifadhi kichakani karibu na nyumbani kwao kisha akajibadili umbo na kuwa paka kisha akaelekea nyumbani. Giza lilikuwa totoro ilikuwa imetimia saa tisa za usiku, pale nyumbani walikuwa wamesinzia usingizi mzito.

Lengo lake la kujibadili katika umbo la paka hakutaka usumbufu wa aina yeyote wakati anaingia nyumbani hapo.

Ndugu msomaji, mungu kamjalia binadamu maarifa mengi, miongoni mwa maarifa hayo ni pamoja na kuchukua maumbo ya vitu pamoja na wanyama mbalimbali.

Katika umbo la paka alilojibadili mtoto huyo, lengo kuu ni kujificha kwa binadamu wenzake ambao hawana taaluma hiyo.

Kwa upande wa wanyama halisi, wenyewe huwa na uwezo wa kuwaona wachawi hata kama watakuwa kwenye maumbo tofauti tofauti.

Mara nyingi mchawi anapochukua umbo la mnyama hupendelea kuwa katika rangi moja, rangi ambayo hupendelewa zaidi ni nyeusi na nyeupe.

Mara chache sana kukuta akiwa kwenye rangi nyekundu au kijivu. Paka wa kichawi hutembea kwa kujiamini sana, pia huwa na rangi moja kama nilivyoeleza.

Paka wa aina hii huwa na macho makali na husisimua mwili unapokutana naye. Si vyema kuwa na tabia ya kuwapiga wanyama nyakati za usiku, kuna muda unaweza kumpiga paka kumbe ni binadamu yakakutokea puani.

Mtoto huyo akiwa kwenye umbo la paka alitokeza kwa mbele ya nyumba hiyo kisha akaelekea kwenye nyumba ambayo hulala.

Wakati huo babu na watu wengine kwenye kaya hiyo walikuwa wamelala usingizi fofofo, aliusogelea mlango ukafunguka kisha akaingia ndani.

Akajibadili katika umbo la binadamu kisha akaweka vifaa vyote vya kichawi mahali salama. Baada ya hapo alichukua dawa na kujipaka ili kuondoa mikosi yote aliyokutana nayo wakati wa mizunguko yake usiku kucha.

Mle chumbani hakukuwa na mtu yeyote, alichukua shuka yake na kupangusa kitanda chake kisha akajilaza.

Wakati huo ilikuwa yapata saa tisa na dakika ushee, alijifunika shuka gubigubi usingizi ukamchukua akazama kwenye bahari ya ndoto mbalimbali.

Miale ya jua la saa mbili ilipenya ndani ya chumba alichokuwa kalala mtoto huyo. Nyumba yenyewe ilikuwa ya miti na fito huku imekandikwa kwa kwa udongo wa mfinyanzi, kwa kuwa nyumba ilikuwa ya muda mrefu fito zilianza kuchoka na baadhi ya madongo yalidondoka chini.

Kupitia nyufa hizo miale ya jua iliweza kupenya moja kwa moja hadi ndani. Kwa jamii ya wafugaji mazingira hayo wanaoyafahamu, huwa ni maisha fulani ya furaha sana.

Mtoto huyo alishituka toka usingizini, taratibu alishusha miguu yake chini ya ardhi. Nyumba yenyewe haikuwa na sakafu, vumbi lilitawala ndani ya nyumba hiyo.

Alichukua nguo zake akavaa kisha miguuni akatinga viatu vya katambuga, viatu hivi ni mashuhuri sana kwa jamii ya wafugaji.

Hutengenezwa kutokana na matairi ya gari, viatu hivyo ni imara na humruhusu aliyevaa kupita mahali popote pasipo kuchomwa na miiba au vitu vyenye ncha kali.

Baada ya hapo alisogea karibu na mlango, akaondoa kitasa kisha akauvuta kwa ndani akatokeza kwa nje.

Pale nje kulikuwa na kundi kubwa la watu waliokuwa wamekuja kumtafuta, kila mmoja alishangilia alipomuona mtoto huyo akitoka ndani.

Kelele za furaha zilisikika kwa kila mtu aliyekuwa eneo hilo, babu yake na mtoto THE BOMBOM alimkimbilia mjukuu wake na kumkumbatia.

Mtoto huyo naye alimkumbatia babu yake kisha wakaanguka chini, kundi la watu waliokuwa kwenye mji huo walishuhudia mapenzi ya babu na mjukuu wake.

Babu alikuwa kamkumbuka mjukuu wake kipenzi, mjukuu aliyezaliwa kutokana na mama yake kubakwa.

Mbali ya kubakwa mama yake pia mama huyo alikuwa kichaa ambaye alifariki mara tu baada ya kumzaa mtoto huyo.

Kwa upande wa baba yake, yeye aliuawa na wananchi wenye hasira kali baada ya tukio la kumbaka kichaa huyo.

Kwa hiyo Mtoto THE BOMBOM amelelewa na babu na bibi kizaa mama kwa muda huo hadi bibi yake alipofariki akabaki na babu yake.

Kwa namna hiyo mtoto huyo alimpenda babu yake kuliko maelezo, ni mtu pekee aliyekuwa akimlea kwa wakati huo huku akimhudumia mambo kadha wa kadha.

Japo walikuwepo wajomba na mama zake wakubwa kwa wadogo, lakini mapenzi yake yalizama kwa babu yake.

Baada ya kuzungumza mambo mbalimbali na babu yake, mtoto huyo aliwasogelea makutano waliokuwa wamekuja nyumbani hapo.

Kabla hajawafikia makutano alishangaa kuwaona mbwa wa nyumbani hapo wakimkimbilia kwa furaha, walipiga magoti mbele yake huku mikia yao wakichezesha chezesha.

Mbwa hao walionekana kumpenda mtoto huyo, wakati mikia yao wakiichezesha chezesha pia masikio yao yalikuwa yakicheza.

Wakati hayo yakiendelaa kuku, bata na njiwa nao walikuja eneo hilo huku wakitamani kumgusa mtoto huyo.

Mambo hayo yalifanyika asubuhi kweupe kila mtu akishuhudia, ndege hao walionekana kufurahia ujio wake maana ni zaidi ya juma moja walikuwa hawajamuona.

Ng'ombe, punda, mbuzi na kondoo walikuwa wakipambana kuvunja mazizi yao ili wamlaki mtoto huyo, kwa kulibaini hilo mtoto huyo aliamua kupita kwenye mazizi hayo angalau awasalimie wanyama hao.

Wanyama hao walionekana kufurahia kitendo hicho, wakabaki wakirukaruka kwa furaha. Alipokamilisha kuwasalimia wanyama hao, hali ikarudi kawaida si mbuzi wala si kondoo waliendelea kusumbua.

Si kuku, si njiwa wala si bata wote walilidhia kumuona mtoto huyo kisha wakamuacha akaendelea kuzungumza na makutano.

Wale walinzi wake watano walipoachana naye mtoto Nabii THE BOMBOM kule kwenye mji wa Kanyama eneo la mlima Makamelwa, walikwenda moja kwa moja nyumbani kwao mtoto huyo.

Walipanda gari na kushuka kituo kijulikanacho Ilongo, wakaulizia kwa watu waliokuwa wanafahamu nyumbani kwao mtoto huyo.

Pale Ilongo walikuta kundi kubwa la watu waliokuwa wakimtafuta mtoto huyo, baada ya kuwaona wale walinzi wake waliamua kuambatana nao hadi nyumbani hapo.

Watu waliendelea kumiminika nyumbani hapo mithili ya siafu kila uchwapo, walikuja, wakaja, wakaja na kufanya kundi la watu wasiyo na idadi.

Hadi hapo ilikuwa imetimia saa tatu asubuhi, mtoto huyo aliwasogelea na kuwasalimia kwa salamu ya kiimani.

"Ukuu wa Mababu zetu" makutano kwa pamoja wakajibu " *Udumu Milele "* kisha akaendelea, "ndugu zangu wana wa mungu karibuni sana nyumbani kwetu. Nimefarijika kwa kiasi kikubwa kuwaona mahali hapa, hii yote ni kwa sababu mnaniamini mimi pamoja na mungu wangu aliyenituma kuja kuokoa kizazi hiki." Alipofika hapo alinyamaza kidogo akakohoa kidogo Kho! Khoo! Kisha akaendelea.

"Ndugu zangu, mungu wangu wa Afrika ambaye ndiye mkuu kuliko mungu wote amenituma kuja kuokoa kizazi hiki. Poleni sana na manyanyaso mnayofanyiwa na watu weupe. Dunia ya leo haikaliki kulingana na mioyo ya hovyo ya watu walioiteka.

"Watu hao wamekuwa wakitengeneza magonjwa ya kuwasigina ninyi watu weusi, hawahitaji kuona kizazi chenu kikisimama imara. Wametengeneza magonjwa mbalimbali kwenye maabara zao wakiwa na lengo la kuangamiza kizazi chenu."

Makutano walikuwa kimya wakisikiliza mafundisho ya mtoto huyo, alichokuwa akizungumza kiliwafanya makutano kutokwa machozi.

Ilikuwa kweli tena kweli tupu, bahati nzuri idadi kubwa ya makutano hao walikuwa watu wazima. Hivyo kilichokuwa kikizungumzwa kiliwaingia akilini, mtoto huyo aliendelea.

"Asilimia themanini ya magonjwa yanayowaangamiza Waafrika yametengenezwa na watu weupe. Ndugu zangu ugonjwa wa UKIMWI haukuletwa na mungu wetu mkuu wa Afrika, ugonjwa huu uliletwa na wafuasi wa shetani wakiwa wamelenga kuwasigina watu weusi miaka ya themanini hasa baada ya uhuru wa nchi za Afrika.

"Watu hawa wamekuwa wakifanya biashara kwa kutumia viwanda vyao kwa kutengeneza mipira ya kike na kiume, vidonge vya kurefusha siku za kuishi na vifaa mbalimbali vinavyotumika kupima ugonjwa huu.

"Katika nchi zao ugonjwa huo haupo. lakini kwenye nchi wanazoziita za ulimwengu wa tatu umekita mizizi.

"Yote hii ni hujuma kwa watu wa rangi nyeusi, bahati mbaya sana wengi mmewaamini na kufuata tamaduni na imani zao za uongo na kishenzi."

Alichukua kiganja chake cha kushoto akapangusa michirizi ya machozi kisha akaendelea, "Wanawaita ninyi mmelaaniwa kutokana na mtoto wa kike wa mtu mweupe kumchungulia baba yake akiwa tupu!.

Huu ni uongo! Ni uongo! Tena uongo mtupu. Kama ni hivyo mbona Waafrika waliolaaniwa na mungu wetu Mkuu wa Afrika hawakuzaa watoto weupe? Huu ni udhalilishaji na ubaguzi mkubwa kwa kizazi cha mtu mweusi! Ukiangalia picha za watakatifu wao huwa ni watu weupe, lakini Shetani ni Mtu mweusi! Na bado mnatukuza imani zao zinazowabagua.

Alitulia kidogo kupima kama aliyokuwa akiyasema walikuwa wakimuelewa. Kisha akaendelea "Ndugu zangu mungu Mkuu wa Afrika kanituma kuwaeleza pia juu ya ufirauni unaotangazwa na hawa mbwa, " mungu wao tayari kawaruhusu kutangaza masuala ya ushoga na usagaji kuwa ni haki za binadamu.

Hawa ni wafuasi wa shetani kabisa, kuendelea kukubaliana na ushenzi wao ipo siku mtaambiwa kuoa au kuolewa na mama au baba zenu ni haki za binadamu.

Mungu wangu mkuu wa Afrika kanituma kuja kuwasisitiza kuwa, mpango huo umelenga kupunguza idadi ya watu duniani hasa watu weusi.

Ipo nia ovu kubwa nyuma ya pazia ambayo inalenga kukididimiza kizazi cha mtu mweusi kupitia upumbavu huu" kwa nini mungu wao anakuwa kigeugeu? Wanyama wa porini kama kenge, fisi, tembo, pundamilia walikuwa eneo wakisikiliza mafundisho hayo ya mtoto THE BOMBOM.

Wadudu kama vipepeo, nyuki, siafu, sisimizi, papasi, ruba nao walikuwepo. Cha kushangaza kila aliyehudhuria mafundisho hayo alikuwa akielewa, hata wadudu na wanyama walipata utambuzi wa lugha hiyo iliyotumiwa na mtoto Nabii THE BOMBOM.

Ndugu msomaji mtoto THE BOMBOM ndiyo kwanza kaanza kufundisha makutano juu ya neno la mungu wake. Je, nini kitampata mtoto huyo katika mafundisho yake? Usikose kufuatilia kisa hiki cha kusisimua sehemu inayofuata.

BASAGALA NHO

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news