Tanzania na India zakubaliana kuimarisha ushirikiano

DAR ES SALAAM-Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na Jamhuri ya India zimekubaliana kuanzisha maeneo mapya ya ushirikiano katika sekta za biashara na uwekezaji, nishati, elimu, maji, afya, tehama na ulinzi.
Makubaliano hayo yameafikiwa na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Stergomena Tax (Mb.) na Waziri wa Mambo ya Nje wa India, Mhe. Dkt. Subrahmanyam Jaishankar (Mb.) katika Mkutano wa 10 wa Tume ya Pamoja ya Kudumu kati Tanzania na India uliofanyika jijini Dar es Salaam.

Akizungumza na waandishi wa habari baada ya Mkutano huo, Dkt.Tax amesema, wameona kuna haja ya kuongeza ushirikiano katika eneo la biashara na uwekezaji ili kukuza uchumi wa mataifa hayo kwa kuwa India ni mbia mkubwa wa Tanzania kibiashara akiwa katika nafasi ya nne na mbia pia wa uwekezaji akiwa katika nafasi ya tano. 
“Tumeona kuna haja ya kuongeza ushirikiano katika sekta za biashara na uwekezaji ili kukuza uchumi wa pande zote mbili, na tumelekeza changamoto zinazoikabili sekta ya bishara na uwekezaji zifanyiwe kazi kwa uharaka na kuondolewa,”ameongeza Dkt.Tax.

Dkt.Tax ameongeza kuwa, pamoja na mafanikio hayo, kuna haja ya kuongeza ushirikiano katika eneo la biashara na uwekezaji ili kukuza uchumi wa mataifa hayo.

Pamoja na mambo mengine, Waziri Tax aliongeza kuwa uamuzi wa Serikali ya India kufungua tawi la Taasisi ya Teknolojia ya India (IIT), Zanzibar utasaidia kujengea uwezo, ubunifu na teknolojia kwa Watanzania.
“Taasisi hii ni taasisi ya kwanza ya teknolojia kuanzishwa na India nje ya taifa lao. Taasisi hiyo itatusaidia kutujengea uwezo, ubunifu na teknolojia na ilikubalika hadi kufikia mwezi Oktoba utekelezaji uwe umeanza,”amesema Dkt.Tax.

Kwa upande wake Waziri wa Mambo ya Nje wa India, Mhe. Dkt. Jaishankar amesema kuwa Mkutano wa 10 wa Tume ya pamoja ya Kudumu kati Tanzania na India umetoa fursa ya kujadili na kuona maeneo mapya ya ushirikiano kati ya mataifa hayo. 
Maeneo hayo ni pamoja na sekta za bishara na uwekezaji, sayansi na teknolojia, mafunzo, afya, kilimo, elimu na ulinzi kwa maslahi ya pande zote mbili. 

“India na Tanzania zimekuwa na ushirikiano wa muda mrefu ulidumu kwa muda mrefu, hivyo ni imani yangu kuwa tutaendelea kushirikiana katika maeneo mapya,”amesema Dkt. Jaishankar.
Akizungumzia kuhusu kuanzishwa kwa Tawi la Taasisi ya Teknolojia ya India-Zanzibar, Dkt. Jaishankar amesema kuwa, kwa mara ya kwanza Serikali ya India imekusuadia kuanzisha tawi la taasisi hiyo Zanzibar ambayo inatarajiwa kuanza rasmi mwezi Oktoba 2023. 
“Tumefurahishwa sana na jambo hili kwani kwa mara ya kwanza taasisi hii inaanzisha tawi lake nje ya India, kuanzishwa kwa tawi la taasisi hiyo Zanzibar ni imani yetu kuwa itasaidia kuboresha elimu na teknolojia nchini Tanzania,” amesema Dkt. Jaishankar.
Makubaliano ya kuanzishwa kwa tawi la Taasisi ya Teknolojia ya India nchini Tanzania yalisainiwa Julai 5, 2023 kati ya Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali, Zanzibar na Taasisi ya IITM pamoja na Wizara ya Elimu ya India.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news