Watano Mtiro Sekondari iliyopo Musoma wabainika kuwa na ujauzito

NA FRESHA KINASA

WANAFUNZI watano wanaosoma katika Shule ya Sekondari Mtiro iliyopo katika Kijiji cha Busekera Kata ya Bukumi Halmashauri ya Wilaya ya Musoma mkoani Mara wamebainika kuwa na ujauzito.
Mkuu wa Shule ya Sekondari Mtiro, Mwalimu Evance Njau ameyasema hayo Julai 26, 2023 kwa Afisa Ustawi wa Jamii Mfawidhi wa halmashauri hiyo, Abel Gichaine aliyefika shuleni hapo akiwa ameambatana na viongozi wa Shirika la VIFAFIO kwa lengo la kuzindua Mwongozo wa Taifa wa Dawati la Ulinzi na Usalama wa Mtoto shuleni na nje ya shule.

Mwalimu Evance amesema, wanafunzi hao wamebainika kufuatia zoezi lililofanyika shuleni hapo la kuwapima ujauzito wanafunzi wa kike kuanzia kidato cha kwanza hadi cha nne ambalo lilifanyika Jumatano ya wiki iliyopita.

"Shule ina jumla ya wanafunzi wote 682,wanafunzi watano walibainika kuwa na ujauzito ambapo kidato cha kwanza ni mwanafunzi mmoja, kidato cha pili wanafunzi wawili, kidato cha tatu mwanafunzi mmoja na kidato cha nne mwanafunzi mmoja. tumeshatoa taarifa ngazi husika,"amesema Mwalimu Evance.

Kwa upande wake Afisa Ustawi wa Jamii Halmashauri ya Wilaya ya Musoma, Abel Ginchaine akizungumza na wanafunzi wa shule hiyo kuhusiana na jambo hilo amewataka kujitambua na kusoma kwa malengo na waachane na tamaa na vishawishi ambavyo vinaweza kuwaletea madhara makubwa ikiwemo mimba na magonjwa ya kuambukiza na hivyo kupoteza ndoto zao.

Ameongeza kuwa, kwa mujibu wa Sheria ya Mtoto namba 21 ya mwaka 2009 imetoa katazo kwa watoto kufanya mapenzi. Na Sheria ya Elimu ya mwaka 1978 Mwanafunzi hatakiwi kufanya mapenzi na pia kwa sheria ya makosa ya kujamiana kufanya mapenzi na mtu chini ya miaka 18 ni ubakaji hivyo waliofanya kitendo hicho wanapaswa kuwajibishwa kisheria bila kufumbiwa macho.

"Niwatake wanafunzi wa kike someni kwa bidii na mhakikishe kwamba mnatimiza ndoto zenu. Msikubali kushawishiwa kwa kupewa vitu vidogo vidogo bora mtembee umbali mrefu kuliko kupata ujauzito na UKIMWI na kupoteza ndoto zenu ambazo mtazifikia iwapo mtakuwa wavumilivu kwa tamaa ya vitu vidogo, nawaombeni sana,"amesema Ginchaine.

Amewataka kutambua kuwa, serikali inatumia fedha nyingi kugharamia elimu bure na ujenzi wa miundombinu bora ya elimu kwa faida yao hivyo watumie fursa hiyo kikamilifu ili waje kuwa msaada kwa taifa kwa siku za usoni.

Ginchaine ameongeza kuwa, tatizo la mimba za utotoni kwa wanafunzi wa kike wanaosoma shule za sekondari za  Halmashauri ya Wilaya ya Musoma ni kubwa ambapo kati ya wanafunzi wa kike 1, 000  zaidi ya wanafunzi 20 wanapata ujauzito kwa kipindi cha miezi sita. Ambapo shule za  Sekondari zikiwa jumla  ni 27, za serikali 25, na 2 za binafsi  za  madhehebu ya dini.

Pia amesema,  taarifa za matukio ya ukatili wa Kijinsia yanayotolewa taarifa Kati ya matukio matatu, tukio moja ni la mimba za utotoni akasema bila kushirikiana wasichana wengi hawatafikia malengo yao kwani watakatisha masomo yao wakati serikali inagharamia elimu bure ili watoto wote wapate haki ya elimu

Diwani wa Kata ya Bukumi Munubi Musa akizungumza na DIRAMAKINI kwa njia ya simu amesema kuwa taarifa hizo alipewa na mwalimu mkuu wa shule hiyo.

"Mimi naona sababu mojawapo zinazochangia hili ni population ya watu eneo hilo ambalo kuna mwingiliano mkubwa wa wafanyabiashara hasa ukizingatia kwamba kuna shughuli za uvuvi watoto wengi wanakuwa huru hawana ulinzi na pia wengine kujihusisha na biashara maeneo hayo inaweza kuchangia.

"Jambo jingine ni usimamizi wa wazazi na walezi kwa watoto, hili pia ni sababu mojawapo unakuta mzazi hafuatilii mtoto wake mienendo yake na tabia kwa karibu. Niombe wazazi wawe karibu na watoto wao kujua tabia zao na pia wawapatie mahitaji yao unakuta mzazi hatoi mahitaji kwa binti yake hii pia inachangia sana kujiingiza katika tabia mbaya na tunapoteza wasomi ambao ni tegemeo kwa taifa letu.

"Sababu nyingine ni wazazi kuwapa jukumu watoto wa kike kufanya biashara kutokana na ugumu wa maisha hii pia ni sababu.

"Lakini niombe wazazi watimize wajibu wao kutoa mahitaji kwa watoto hasa wa kike ambao kimsingi wamekuwa wakishawishiwa sana. Na pale mtu anapobainika kampa mwanafunzi ujauzito wazazi waache tabia ya kumaliza mambo haya kimya kimya badala yake watoe ushirikiano kwenye vyombo vya sheria wahusika wachukuliwe hatua kali," amesema Mheshimiwa Musa.

Afisa Elimu Sekondari wa Halmashauri ya Wilaya ya Musoma, Majidu Kalugendo amesema kuwa, taarifa hizo hajazipata kwa maandishi.

"Wanatakiwa walete taarifa na vithibitisho vya daktari ndipo naweza kusema ni mimba au nini kwa sasa sijapokea taarifa yoyote,"ameiambia Afisa Elimu huyo ameiambia DIRAMAKINI kwa njia ya simu.

Aidha, DIRAMAKINI imemtafuta kwa njia ya simu Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Musoma, Msongela Palela ambapo amesema kuwa, taarifa hizo hazijafika Ofisini kwake na kwamba atazifanyia ufuatiliaji.

"Taarifa hizo ndio nazisikia kutoka kwako nitazifUatilia tu kwa source yako, lakini nashukuru kwa hiyo taarifa nitazifUatilia,"amesema Palela.

Kwa matokeo ya Mock kidato cha nne mwaka huu Mtiro Sekondari daraja la kwanza ni moja, daraja la pili watatu, daraja la tatu 12, daraja la nne 65, na daraja zero 39.

Mmoja wa Wazazi wa Binti aliyepata ujauzito kati ya wasichana watano waliobainika  ambaye ameomba jina lake lihifadhiwe  akizungumza na DIRAMAKINI amesema kuwa, njia ambayo inaweza kusaidia Watoto wa kike wasipate ujauzito ni wazazi kuungana pamoja na Serikali kujenga mabweni ya wasichana shuleni hapo na pia  wataalam wa afya wawape elimu wasichana si tu katika shule hiyo bali shule zote kusudi wajisimamie. 

"Mwanangu akijifungua aendelee na masomo yake ingawa najua kisaikolojia anaweza asiwe vizuri. Lakini nashukuru fursa hii ya Rais kuwapa nafasi ya kurudi shule baada ya kujifungua  nitajitahidi kuwashirikisha Viongozi wa dini wamtie moyo na pia washauri wa kisaikolojia akae vizuri. 

"Nami  mzazi nitatimiza wajibu wangu kikamilifu sasa kumfuatilia kwa karibu tofauti na awali  naamini kosa hili limeshatokea pengine atafanya vizuri.  Mtoto akinyea mkono usafishe kwa maji Safi  sio kuukata," amesema mzazi huyo jina limehifadhiwa. 

Aidha,DIRAMAKINI imefanya juhudi za kumtafuta Askofu Mkuu wa Kanisa la Tanzania Missionary  Revival Church (TMRC) Jimbo la Mara lilipo Kata ya Kigera Wilaya ya Musoma kuzungumzia Jambo hilo kiimani na kijamii,  amesema kuwa pamoja na Serikali kuweka fursa ya wanafunzi wa kike kurudi shule baada ya kujifungua lakini Juhudi za makusudi lazima zifanywe na wazazi  na Jamii nzima  kuwalinda  Watoto wa kike wasipate ujauzito kwani ni kosa mbele za Mungu. 

"Mpango wa Mungu ni kuona watu wakioana kwa kufuata taratibu ambazo Mungu ameziweka,  hapa namaanisha msichana awe mtu mzima amekuwa kiakili na kijana pia  wafanye taratibu za uchumba ndoa ifungwe  wote wakiwa Wana utambuzi wa kile wanachoenda kufanya, kitendo cha hawa Watoto kupewa mimba ni kosa mbele za Mungu maana yake wamezini na uzinzi ni dhambi,"amesema Askofu Lutubija na kuongeza kuwa.

"Niwashauri Viongozi wa dini wenzangu tuimarishe mafundisho ya kiroho kanisani na misikiti  ili Kuzuia maovu kama haya ya Watoto wetu kupewa ujauzito  wakiwa bado wanafunzi ikitokea wengine wasiendelee na masomo  baada ya kujifungua maana yake wamekatisha ndoto zao yawezekana wapo miongoni mwao wangekuja kuwa Waandishi wa Habari kama wewe, waalimu, mahakimu na pia kusaidia Jamii kupitia elimu na utaalamu wao," amesema Askofu Lutubija.  

Rhobi Samwelly ni Mwanaharakati na Mtetezi wa haki za Binadamu ambaye ni Mkurugenzi wa Shirika la Hope for Girls and Women in Tanzania (HGWT) lenye makao makuu yake Mugumu Mjini Wilaya ya Serengeti Mkaoni Mara linalojishughulisha kusaidia na kuokoa wasichana wanaokimbia aina mbalimbali za Ukatili wa Kijinsia  ikiwemo Ukeketaji na ndoa za utotoni akizungumza na DIRAMAKINI kuhusiana na wasichana hao kubainika ni wajawazito amesema.

"Wazazi, walezi na jamii kwa ujumla hivi Sasa Mkazo katika kuimarisha malezi kwa Watoto wa kike umepungua, utakuta Baba na Mama hawazungumzi na watoto wake wa kike kuwapa elimu ya kujilinda na kujitambua. Watoto wa kike wanakumbana na kadhia ya kushawishiwa kama hawana elimu ya kujitambua ni rahisi kushawishiwa,"amesma Rhobi na kuongeza kuwa. 

"Mkazo  wangu kwa Wazazi na walezi tuimarishe malezi tuwape elimu Watoto wa kike wajitambue wao ni kina nani wasikubali kurubunika kwa pesa kidogo, na pia Wazazi tujitahidi kuwapa mahitaji yao ya msingi ikiwemo taulo za kike yawezekana mtoto anachangamoto ya taulo ambayo inauzwa Shilingi 3,000, mzazi asipotoa huyo mtoto atawezajie kujistili wakati wa hedhi?" amehoji na kuongeza kuwa 

 "Kwa  hiyo akikutana na mtu ambaye anampa Shilingi 5000/, lazima atashawishika kusudi apate anachohitaji kutokana na mzazi kushindwa kumtimizia kumbe ndio anadumbukia kwenye mimba na hata  wakati mwingine maradhi sote tuwe  walinzi kusudi tuwaokoe waweze kusoma na kutimiza ndoto zao pasipo kuwawezesha na kuwawekea mazingira bora ni vigumu wao kufikia ndoto kulingana na changamoto zinazowakabili "amesema Rhobi. 

Aidha, Rhobi amesema iwapo hakutakuwa na Mshikamano na umoja  wa wadau, serikali na Wananchi katika kudhibiti mimba za utotoni kwa wanafunzi  ikiwemo kuwakamata wahusika nankuwafikisha kwenye vyombo vya sheria,  Kuna uwezekano mkubwa wa mimba hizo kuongezeka kwa kigezo kuwa baada ya binti kujifungua atarudi kuendelea na masomo, Jambo ambalo ni hatari kwa taifa la kesho.  

Dkt. Joachim Eyembe ni Daktari Bingwa wa Magonjwa  ya Ndani  katika Hospital ya  Rufaa ya Mkoa  wa Mara ambapo akizungumza na DIRAMAKINI baada ya Mwandishi wa Habari hizi kumtafuta kwa njia ya simu amesema madhara ya mimba za utotoni kwa  binti kujifungua katika umri mdogo anaweza kuathirika kisaikolojia kutokana na yeye kuwa 'mtoto' tena analea mtoto ambaye anakuwa amemzaa. 

Pia,Dkt. Eyembe amesema Madhara mengine ni kwamba "uwezekano wa binti kujifungua salama unakuwa mdogo kutokana na viungo vyake vya kike vinakuwa bado havijakomaa kupitisha mtoto kiuno na nyonga. Pia kutokana na viungo vyake kuwa bado havijakomaa Kuna uwezekano pia wa kuchanika na kupoteza damu nyingi hali ambayo inaweza sababisha apoteze maisha."amesema Dkt. Eyembe. 

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news