Mama Mariam Mwinyi asisitiza faida tele za mwani

ZANZIBAR-MKE wa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini wa Zanzibar Maisha Bora Fondation (ZMBF), Mama Mariam Mwinyi, amewashauri Wazanzibari hasa wanawake kutumia mwani kwani una virutubisho vingi vinavyoimarisha afya hasa za mama wajamzito. 
Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini wa Zanzibar Maisha Bora Foundation, Mama Marian Mwinyi (wa pili kulia) akikabidhi kamba kwa wanachama wa moja ya vikundi vya ukulima wa mwani vya wilaya ya Magharibi ‘B’ wakati wa hafla ya ugawaji wa chanja za kuanikia mwani na vifaa vingine vya kuzalishia zao hilo vilivyotolewa na ZMBF kwa ufadhili wa Shirika la Chakula na Kilimo Ulimwenguni (FAO). Wa kwanza kulia ni Mwakilishi Mkaazi wa FAO, Nyabenyi Tupo.

Ameeleza kuwa, hatua hiyo itaimarisha ustawi wa jamii na kupugunza vifo vya mama na watoto vinavyotokea wakati wa uzazi kutokana na wajawazito kupata matatizo ya upungufu wa damu. 

Mama Mariam alieleza hayo katika hafla ya kukabidhi vifaa vya kuanikia mwani kwa wakulima wa mwani Zanzibar iliyofanyika katika uwanja wa mpira Bweleo, wilaya ya Magharibi ‘B’, mkoa wa Mjini Magharibi Unguja. 

Alisema zao la mwani lina faida nyingi vikiwemo virutubisho vinavyosaidia mwanaadamu kuliko virutubisho vinavyopatikana katika bidhaa nyengine hivyo ikiwa kinamama watatumia mwani kikamilifu wataongeza tija kwenye uchumi wao pia. 

“Zao la mwani ni muhimu hapa duniani na kwa maendeleo ya mwanadamu kwa ujumla kwani kwa nyakati hizi faida zake zimeanza kushika kasi ikiwemo ya kuimarisha maisha ya mtu mmoja mmoja na taifa kwa ujumla,”alieleza Mama Mariam. 

Aidha alisema Zanzibar imeanza kulima zao hilo takribani miaka 20 iliyopita na kupongeza juhudi zinazochukuliwa na wadau mbali mbali ikiwemo Serikali ya Mapinduzi Zanzibar ya awamu ya nane kuiendeleza sekta ya mwani. 
“Zao la mwani limeendelea kushika kasi duniani kwani mwani unatumika kama chakula, dawa, mbolea, vipodozi na muhimu kuhakikisha unachakatwa vizuri na katika hali ya usafi hivyo ni lazima wazanzibari tukatumia vyakula vya asili,”alieleza. 

Alibainisha kuwa kwa sasa ukulima wa mwani umerahisishwa hivyo alitoa wito kwa vijana kujihusisha na kilimo hicho ili kuongeza kasi ya uzalishaji wake na kukabili changamoto ya ukosefu wa ajira. 

“Pamoja na mabadiliko ya tabia ya nchi bado ukulima wa mwani ni rahisi kwani unahitaji maji na jua pekee vitu ambavyo Zanzibar vinapatikana kwa asilimia kubwa kama ilivyo duniani ambayo inaweza kulimwa mwani,” alieleza Mama Mariam. 

Alisema, Zanzibar inaongoza katika kilimo cha mwani barani Afrika hivyo aliwatia moyo wananchi na wakulima wa zao hilo na kuwa tayari kulikuza ambapo asilimia 98 ya mwani unaopatikana katika soko la dunia unatoka bara la Asia na asilimia mbili pekee ndio unatoka katika mabara mengine. 

“Hili ni dhahabu yetu tuitunze na taasisi yetu ililiona hilo mapema kuona tuwasaidia wakulima wetu na hatimae kufikia kwenye masoko hivyo nawaasa wajasiriamali na wakulima wa mwani kuhakikisha mnatumia vizuri vifaa mnayopatiwa ili viweze kudumu na kuleta tija,”alieleza. 

Mwenyekiti huyo pia aliipongeza serikali kwa kuipa kipaumbele sekta ya mwani ambayo inasaidia kuwakomboa wakulima wa zao hilo na kuiomba Wizara ya Uchumi wa Buluu na Uvuvi kushirikiana na wadau wengine kuutangaza mwani ili uweze kujulikana na kutambulika duniani kote. 

“Zipo nchi ambazo wanataka bidhaa hizi kama China lakini hazijawafikia na tumeshawaambia tutawakaribisha ili waweze kuja, sasa tujiandae ili kutengeneza bidhaa zenye ubora ili tuweze kuuza nje fursa bado ipo tuongeze juhudi ili kulima mwani mwingi tuuchakate na kuuza ndani ya nchi yetu na nje,” alibainisha. 

Aidha aliipongeza FAO na Wizara ya Uchumi wa Bluu kuiunga mkono taasisi hiyo katika kuwasaidia wakulima ili waweze kuongeza tija na kujikwamua na umasikini. 

Naye Katibu Mkuu Wizara ya Uchumi wa Baluu na Uvuvi,Dk. Suleiman Aboud Jumbe, alisema hayo ni matumaini mapya ya uchumi wa bluu kupitia sekta ya mwani kwa wakulima waliofadhiliwa na FAO chini ya wizara. 

Alimpongeza Mama Maryam kwa juhudi kubwa anazozichukua kujitolewa kuwasaidia wanawake na kinamama katika nyanja mbalimbali za kiuchumi, kijamii, kiafya na kimaendeleo hapa Zanzibar na kuweza kuleta mabadiliko chanya ya kuinua sekta ya mwani ambayo ni nguzo ya sekta ya uchumi wa bluu na kimbilio kwa wananchi wanaojikita katika zao hilo. 
Mapema Mwakilishi Mkaazi wa wa Shirika la Kilimo la Umoja wa Mataifa (FAO), Nyabenyi Tipo, alipongeza serikali ya SMT na SMZ kwa kusaidia jamii kuondoa changamoto za kiuchumi kupitia sekta ya mwani kama sehemu ya utekelezaji wa malengo endelevu ya dunia. 

Alisema FAO imesaidia kwa kiwango kikubwa harakati za serikali katika kuweka mkazo kusaidia na kujenga afya uchumi na maendeleo endelevu ya wakulima na wananchi wa Tanzania kwa kutoa elimu, kufanya utafiti na kutoa vifaa kwa wakulima wa zao ili kuongeza tija kwa zao la mwani. 

Hivyo, aliahidi kwamba FAO itaendelea kusaidia wakulima wa mwani katika maeneo mbali mbali kwa lengo la kuongeza thamani ya mwani na kukabiliana na changamoto za mabadiliko ya tabia ya nchi. 

“FAO inatambua mchango na kazi kubwa inayofanywa na ZMBF na juhudi za SMT na SMZ katika kuwaendeleza wakulima wa mwani hasa kwenye eneo la kuongeza thamani ya zao hilo ili tija ipatikane,”alisema. 

Akitoa salamu za ZMBF katika hafla hiyo, Ofisa Mtendaji Mkuu wa taasisi hiyo, Fatma Fungo, alisema ndani ya mwaka mmoja tokea kuzinduliwa kwa taasisi hiyo mwaka jana wameweza kutambua na kuwashika mkono vikundi 18 vya wakulima wakiwemo kinamama na vijana Unguja na Pemba. 

Alisema awamu ya kwanza ilijumuisha kusaidia mahitaji ya vifaa vya kilimo kwa ajili a mahitaji ya uzalishaji wa mwani bora wenye viwango ambapo kupitia ama hiyo jumla ya boti za faiba tisa zenye urefu wa mita tano na mashine zenye uwezo wa 9.9 HP na maboya ya ukozi ambavyo viligaiwa kwa vikundi hivyo. 

Hata hivyo, alisema chamgamoto ya teknologia rafiki za kusarifu zao hilo haikusahaulika kutatuliwa ambapo ZMBF ilifadhili mashine za kusagia mwani sita, mashine za kukorogea sabuni sita na vifaa vyengine vya kusarifu ambapo vifaa hivyo vilikuwa na thamani ya zaidi ya milioni 130. 

Sambamba na hayo, alisema katika kufanya tathmini na maendeleo ya vikundi vya wakulima hao vifaidika changamoto ya ubora wa mwani baada ya kuvunwa ilibainika wakati wa uanikaji kwani wakulima wengi huanika chini na kupelekea mwani huo kuingia uchafu na kuharibika na maji kipindi cha mvua na kupelekea zao hilo kupoteza ubora na kumpa hasara mkulima. 

“Kwa kushirikiana na FAO na wadau wengine tumetengeneza chanja za kuanikia mwani 220 zenye urefu wa mita sita na upana wa mita mbili zina uwezo wa kukaushia mwani kwa siku moja hadi mbili zenye thamani ya zaidi ya shilingi milioni 200 lakini pia kamba 150 zimegaiwa kwa vikundi vya wakulima hawa Unguja na Pemba,”alieleza. 

Mmoja wa wanufaika wa vikundi vya mwani Zanzibar, Safia Hashim Makame, kutoka Bweleo aliipongeza taasisi hiyo kwa kuwaona wakulima wa mwani kwani walikuwa wakipata tabu katika kuendesha kilimo hicho hivyo hivi sasa wanaamini kilimo hicho kitapata soko la kujikomboa kiuchumi. 

Alisema awali walikuwa wakianika mwani siku tatu lakini hivi sasa kupatiwa vifaa hivyo wataweza kuanika kwa siku moja vitasaidia kuinua kilimo chao ambacho kwa kiasi kikubwa wanakitegemea katika kujikimu kimaisha. 

Vifaa vilivyotolewa katika hafla hiyo ni pamoja na chanja za kuanikia mwani, maturubali na vyavu kwa vikundi vya wakulima wa mwani vilivytolewa na ZMBF kwa kushirikiana na FAO.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news