Serikali yapewa saluti uwekezaji matibabu ya moyo nchini

DAR ES SALAAM-Mmoja wa Madaktari bingwa wachache duniani wanaofanya upasuaji mgumu wa moyo kwa watoto Prof. Tomasz Mroczek kutoka Chuo Kikuu cha Jagiellonian cha nchini Poland ameipongeza Serikali kwa kusomesha wataalamu wa moyo na kununua vifaa tiba vinavyotumia teknolojia ya kisasa.

Prof. Mroczek alizitoa pongezi hizo hivi karibuni wakati akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya kumalizika kwa kambi maalumu ya siku tano ya matibabu ya magonjwa ya moyo kwa watoto waliyoifanya katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI).

Prof. Mroczek alisema hii ni mara yake ya kwanza kufika hapa nchini na walikuja kuona namna ambavyo madaktari wa JKCI wanavyofanya upasuaji wa moyo na kuangalia jinsi watakavyoweza kushirikiana katika kufanya upasuaji mgumu zaidi.

“Kitu nilichokitegemea kukikuta siyo nilichokikuta hapa, nimekuta madaktari wanafanya upasuaji mgumu wa kurekebisha mishipa ya damu ya moyo ambayo haijakaa katika mpangilio wake kwa kutumia muda mfupi.

"Tofauti na nchi zingine nilizokwenda pia kuna wataalamu wazuri na vifaa tiba viko vya kutosha na vya kisasa vinavyoenda na teknolojia ya matibabu ya moyo inayotumika katika nchi zilizoendelea.

“Nimekutana na watalamu wazuri ambao tumefanya nao upasuaji wa moyo kwa watoto wenye matatizo ya moyo ya kuzaliwa nayo ninaamini ushirikiano huu utakuwa endelevu ili sote kwa pamoja tuweze kuwahudumia watanzania wenye matatizo ya moyo,”alisema Prof. Mroczek.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI), Dkt. Peter Kisenge aliwashukuru wataalamu hao kutoka nchini Poland ambao walifanya upasuaji mkubwa kwa watoto na mdogo kwa watu wazima na kusema kuwa ujio wao unaenda kufungua milango ya mafunzo kwa madaktari hapa nchini. 

Dkt. Kisenge ambaye pia ni daktari bingwa wa moyo alisema kwa muda wa siku tano ambao madaktari hao walikuwepo katika Taasisi hiyo wameweza kufanya upasuaji mgumu wa moyo na kutoa mafunzo na ujuzi kwa wataalamu wa JKCI.

“Tulisaini makubaliano na wenzetu wa Chuo Kikuu cha Jagiellonian cha nchini Poland ya kushirikiana katika mafunzo, tafiti na kufanya matibabu.

"Ushirikiano huu umeanza kufanya kazi na utakwenda kufungua milango ya kufanya tafiti mbalimbali zitakazoleta manufaa."

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news