BABA JAKAYA KIKWETE, HAPI BETHIDEI KWAKO!

NA LWAGA MWAMBANDE

OKTOBA 7, 1950 alizaliwa Rais mstaafu wa Awamu ya Nne wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete.

Dkt.Kikwete alizaliwa huko Msoga Mkoa wa Pwani akiwa mtoto wa sita katika familia ya watoto tisa. Mwaka 1976 alijiunga na Chuo Kikuu cha Maofisa wa Jeshi Monduli na kutunukiwa Cheo cha Luteni Kanali na baadaye kuwa Mkufunzi Mkuu na Kamisaa wa Siasa katika chuo hicho.

Mheshimiwa Dkt.Kikwete alifanya kazi katika Chama Cha Mapinduzi kwa nyadhifa mbalimbali kwenye mikoa ya Singida na Tabora na wilaya za Nachingwea na Masasi.

Aidha, mwaka 1988 aliteuliwa kuwa Mbunge na Naibu Waziri wa Nishati na Madini. Mwaka 1990 alichaguliwa kuwa Mbunge wa Jimbo la Bagamoyo na akateuliwa kuwa Waziri wa Wizara ya Maji, Nishati na Madini.

Nyadhifa nyingine alizoshika ni Waziri wa Fedha mwaka 1994 na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa kuanzia mwaka 1995 hadi 2005.

Alishika rasmi wadhifa wa urais mwaka 2005 na kuchaguliwa tena 2010 kwa muhula mwingine wa miaka mitano.

Mheshimiwa Dkt.Jakaya Kikwete ikiwa leo ni siku yake ya kuzaliwa, Watanzania na Dunia inajivunia mchango wake katika nyanja mbalimbali hususani upande wa diplomasia ambapo amebobea, hivyo licha ya kustaafu nafasi ya urais bado ameendelea kuhudumu katika taasisi na mashirika mbalimbali ya Kimataifa.

Mshairi wa kisasa, Lwaga Mwambande anasema kuwa, kuna mengi ya kujifunza kutoka kwa Mheshimiwa Dkt.Jakaya Mrisho Kikwete. Endelea;

1. Miaka sabina tatu, hapi bethidei kwako,
Ewe kiongozi wetu, twafurahi siku yako,
Sherehe yako ni yetu ukikata keki yako,
Baba Jakaya Kikwete, hongera kwa kumbukizi.

2. Maisha yako kitabu, ni cha kwetu si cha kwako,
Kongole bila aibu, maisha na kazi yako,
Kwetu wewe wa karibu, katika maisha yako,
Baba Jakaya Kikwete, hongera kwa kumbukizi.

3. Rais wetu wa nne, limaliza muda wako,
Lakini yako matone, hiyo kumbukumbu yako,
Siasa bora na nene, zilitamalaki kwako,
Baba Jakaya Kikwete, hongera kwa kumbukizi.

4. Pamoja yote mengine, hili kubwa sana kwako,
Chuo kikuu kingine, ule uasisi wako,
Udom chetu kinene, hiyo ni alama yako,
Baba Jakaya Kikwete, hongera kwa kumbukizi.

5. Wewe ni mtu wa watu, hiyo ni tabia yako,
Mcheshi kwao na kwetu, hiyo ndiyo jadi yako,
Mtu unajali utu, hayo ni maisha yako,
Baba Jakaya Kikwete, hongera kwa kumbukizi.

6. Japo umepumzika, urais siyo wako,
Ni mzee wahusika, kumwaga hekima yako,
Siku zinavyokatika, tushibe maneno yako,
Baba Jakaya Kikwete, hongera kwa kumbukizi.

7. Miaka sabina tatu, twatoa hongera kwako,
Maneno kutoka kwetu, baraka zizidi kwako,
Twamuomba Mungu wetu, atunze maisha yako,
Baba Jakaya Kikwete, hongera kwa kumbukizi.

8.Twakuombea kwa Mungu, azidishe afya yako,
Akuepushe machungu, furaha ijae kwako,
Kukitokea kiwingu, hicho kisifike kwako,
Baba Jakaya Kikwete, hongera kwa kumbukizi.

9. Na leo Mama Salma, aioke keki yako,
Akate kipande chema, ule kwa furaha yako,
Tukipata picha vema, tufurahi siku yako,
Baba Jakaya Kikwete, hongera kwa kumbukizi.

10. Jakaya sabina tatu, leo ndio myaka yako,
Kitabu chako ni chetu, kuhusu maisha yako,
Ndio twasoma kivyetu, na watangulizi wako,
Baba Jakaya Kikwete, hongera kwa kumbukizi.

Lwaga Mwambande (KiMPAB)
lwagha@gmail.com

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news