Tanzania yang'ara Ripoti ya Benki ya Dunia ya Ukomavu wa Matumizi ya Teknolojia

NA GODFREY NNKO

WAZIRI wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari,Mheshimiwa Nape Nnauye amesema, hadi sasa Tanzania imeorodheshwa kwenye Ripoti ya Benki ya Dunia ya Ukomavu wa Matumizi ya Teknolojia 2022 kuwa ni ya kwanza kati ya nchi za Afrika Mashariki na ya pili kwa Bara la Afrika.

"Kuna kazi kubwa ambayo imefanyika, ya kuifanya Tanzania iwe tayari kutumia teknolojia hizi ibukizi ndiyo maana kongamano hili ni la muhimu kuendelea kutuweka kwenye ramani.

"Kama ni ya kwanza kwa ukanda wetu wa Afrika Mashariki na ya pili katika Bara la Afrika bila shaka tunakwenda vizuri, niwashukuru sana ambao wamechangia kuifikisha nchi yetu hapa ilipofika."

Mheshimiwa Waziri Nape ameyasema hayo leo Oktoba 17, 2023 katika ufunguzi wa Kongamano la Saba la Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) nchini ambalo linaendelea katika Ukumbi wa Mikutano wa Kimataifa wa Mwalimu Julius Nyerere (JNICC) jijini Dar es Salaam.

"Kongamano hili linatumika kama jukwaa muhimu kwa wadau wote wa TEHAMA nchini kuja pamoja, kubadilishana mawazo na kuchunguza fursa katika Sekta ya TEHAMA."

Amesema, makongamano haya yatakuwa na maana kubwa kama kila mwaka watafanya tathimini ya kina wa waliyokubaliana katika kongamano lililopita.

Lengo la kufanya tathimini hiyo, Mheshimiwa Waziri Nape amesema, ni ili kuona ni kwa kiasi gani wametekeleza waliyokubaliana, vikwazo walivyokutana navyo na namna ya kuvitatua ili waweze kusonga mbele.

"Muhimu kuweka malengo ili tupige hatua, na kutumia malengo hayo kujipima kila wakati. Nichukue fursa hii kwa kuwapongeza kwa kuandaa kongamano hili tena, na niwashukuru wote ambao wametenga muda wao kuja kuhudhuria hapa.

"Niwashukuru waliodhamini kongamano hili, asanteni sana, ni matumaini yangu kadri tunavyosonga mbele wadhamini wataongezeka zaidi, na mimi niwaahidi nitaweka nguvu ya kutosha kuona namna ambavyo tunaongeza udhamini."

Vile vile, Mheshimiwa Waziri amewapongeza waandaji wa kongamano hilo kwa namna ambavyo wameweka ratiba vizuri ambapo kongamano hilo lina siku tano.

"Mmeanza na wanawake, na takwimu zinaonesha ushiriki wa wanawake kwenye TEHAMA duniani siyo mzuri sana, kwa hiyo uamuzi wa kuwa na siku yao maalumu utasaidia kuongeza ushiriki wao.

"Lakini, mmeweka vijana, niwaombe safari ijayo kwa sababu katika makundi ambayo yanaonekana yapo nyuma ni ya wanawake, vijana na wenye ulemavu. Kwa hiyo tuone namna kongamano lijalo tuwe na siku ya wenye ulemavu, tuzungumze namna ambavyo ushiriki wao utaongezeka."

Mheshimiwa Waziri Nape amesema, kama ilivyo kauli mbiu ya kongamano hilo, "Kutumia Teknolojia Ibukizi katika Mapinduzi ya Kidigitali ili Kuzalisha Ajira na kuleta Maendeleo ya Kiuchumi na Kijamii" ana imani kuwa,ushirikiano, majadiliano, mazungumzo yatakayofanyika yataunda mustakabali wa pamoja wa sekta hiyo.

"Na kutumia teknolojia hizi zinazoibukia kulingana na matakwa ya raia wetu, maadili na tamaduni zetu. Ninafahamu kuna changamoto mbalimbali za matumizi ya teknolojia hizi zinazoibukia.

"Hata hivyo, ni muda mwafaka kushiriki katika mijadala yenye maana ambayo itafungua njia kutumia teknolojia hizi kiufanisi zaidi.

"Kwa kutumia maarifa, na uzoefu wetu wa pamoja nina imani kwamba tunaweza kuzishinda na kufungua uwezo mkubwa ulio ndani ya wataalamu hawa wa TEHAMA ambao tunakutana.

"Ni wito huu wa umuhimu, napenda kuwahimiza washiriki kutumia fursa hii kuchangia kikamilifu, kubadilishana maarifa, kukuza ushirikiano na kuweka msingi mzuri wa mustakabali wa Sekta ya TEHAMA hapa nchini.

"Kama mnavyofahamu, wiki iliyopita Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt.Samia Suluhu Hassan alifanya zaiara huko nchini India, katika ziara hii Mheshimiwa Rais ameonesha nia thabiti ya kuipeleka nchi hii katika jamii iliyobadilika yenye misingi ya maarifa, itakayoifanya nchi kufikia mapinduzi ya nne na ya tano ya viwanda.

"Kutokana na maono haya, tarehe 10 mwezi Oktoba, 2023 wizara yetu imesaini mkataba wa mashirikiano na Wizara ya Masuala ya Kielekroniki ya India, kushirikiana katika kubadilishana ujuzi na utaalamu wa teknolojia mbalimbali katika eneo la kidigitali pamoja na teknolojia hizi ibukizi."

Amesema, katika mikataba na makubaliano yaliyofikiwa na India, mmoja wapo ni kwa ajili ya kushirikiana na wenzao wa India kwenye ubunifu hususani kwenye teknolojia ambazo zinaibukia.

"Nachukua nafasi hii kuwasihi mtumie fursa za makubaliano hayo, kujenga uwezo na kupata uzoefu ili tuifanye Tanzania, kitovu cha teknolojia bunifu kwa ukanda wetu kwa na hata Bara la Afrika.

"Mashirikiano haya yanalenga kufikia maono yaliooneshwa kwenye mkakati wa uchumi wa kidigitali ambao umeandaliwa na wizara yangu, kwa kushirikiana na wadau wa sekta ya umma na binafsi, na tuko hatua za mwisho, mkakati huu sasa utapelekwa kwenye vikao vya maamuzi kwa ajili ya kuanza kutumika."

Amesema, mashirikiano hayo na wenzao wa India na mengine kutoka nchi mbalimbali duniani yataendelea kuboresha ukomavu wa Tanzania kwenye matumizi ya teknolojia katika kutoa huduma kwa wananchi.

"Kulingana na Ripoti ya Teknolijia na Ubunifu inayotolewa na Taasisi ya Umoja wa Mataifa inayolenga kukuza biashara ya Kimataifa hasa baina ya nchi za viwanda na nchi zinazoendelea ya mwaka 2022 imeonesha India imeshika nafasi ya 46 katika ubunifu wa teknolojia za kisasa wakati Tanzania tukiwa nafasi ya 146.

"Hivyo, kufanya mashirikiano na nchi zilizopiga hatua zitachangia katika kufanikisha malengo tuliyojiwekea, India ni mfano, lakini ninajua tumekuwa tukishirikiana na nchi nyingine ambazo zimepiga hatua kubwa, na mimi nina matumaini makubwa kwamba tutajifunza kutoka kwao, tuchukue uzoefu kwao, lakini tunakokwenda tunataka tuipeleke Tanzania iwe nchi kiongozi kwenye ukanda wetu na Bara la Afrika.

"Na Dunia itambue tunayo kila sababu,kwamba mazingira yanaruhusu, amani na utulivu tulio nao, utashi wa kisiasa uliopo, uwekezaji uliowekwa kwenye miundombinu hatuna sababu ya kubaki nyuma.Ni matumaini yangu kongamano hili litakuwa changamoto tosha ya kutufanya tupige hatua."

Awali, Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) nchini, Dkt.Nkundwe Mwasaga amesema, hilo ni kongamano la saba la TEHAMA nchini.

Dkt.Mwasaga amesema, hilo ndiyo kongamano kubwa la TEHAMA nchini ambalo linawakutanisha wadau mbalimbali wa TEHAMA kutoka ndani na nje ya nchi.

"Kongamano hili ni tofauti na makongamano mengine sita yaliyopita, limekuwa ni la siku tano, Jumatatu tulijadiliana kuhusiana na mafanikio na changamoto zinazowakuta wajasiriamali wanawake katika TEHAMA, na tulikuwa na mada nane tulizozijadili.

"Mada hizo ziligusa mambo mbalimbali, tulikuwa tunagusa mambo ya jinsi ya kupata mitaji kwa kampuni zinazoongozwa na wanawake, tulikuwa tunaangalia masuala ya uwekezaji katika kampuni za wanawake barani Afrika.

"Tuliangalia pia, kauli mbiu ya kongamano hili inawagusa vipi wanawake na watoa mada wote na waongoza mada kwa kiasi kikubwa ninaweza kusema takribani asilimia 85 walikuwa ni wanawake wenyewe.

"Tumepata vitu vingi sana, tofauti na makongamano mengine yaliyopita. Siku ya pili tulijadiliana kuhusiana na mafanikio na changamoto mbalimbali wanazokutana nazo vijana."

Dkt.Mwasaga amesema, sababu za kuwa na siku hizo mbili ni kwa sababu Taifa linaelekea katika ujenzi wa uchumi wa kidigitali jumuishi, hivyo kwa kufanya hivyo inabidi wayaangalie makundi hayo muhimu mawili.

"Kwa sababu, tafiti mbalimbali zimeonesha kwamba, tukiweza kuwafanya wanawake na vijana wawe na mafanikio katika TEHAMA tutapata ule ukuaji ambao unachagizwa na TEHAMA vizuri zaidi.

"Kwa sababu Tanzania ina bahati ya kuwa na vijana wa miaka kuanzia 15 hadi 34 ambao ni takribani asilimia 33 ya idadi ya Watanzania.Na hao ni kama milioni 21, kwa hiyo hizo ndiyo siku mbili."

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news