Waziri Dkt.Jafo azindua Mwongozo wa Ukaguzi wa Mazingira Miradi ya Ujenzi

DODOMA-Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Mhe.Dkt.Selemani Jafo amelitaka Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) kuongeza wigo wa kuandaa Miongozo ya Tathimini ya Athari za Mazingira (TAM) kupitia sekta za viwanda,nishati, kilimo na maji ili kuharakisha zoezi la mapitio ya miradi ya tathimini za athari kwa mazingira.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Dkt. Selemani Jafo (wa tatu kutoka kulia) pamoja na Watendaji na Viongozi wa Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) na Kituo cha Kituo cha Sayansi na Mazingira cha Nchini India (CSE) wakionesha nakala ya mwongozo wa ukaguzi wa Mazingira kwa Miradi ya Ujenzi wa Majengo muda mfupi baada ya uzinduzi wa mwongozo huo. Hafla hiyo ilifanyika leo Jumatano (Oktoba 18, 2023) katika Mji wa Serikali, Mtumba Jijini Dodoma.

Akizungumza leo Jumatano ya Oktoba 18, 2023 jijini Dodoma katika hafla ya uzinduzi wa mwongozo wa ukaguzi wa mazingira kwa miradi ya ujenzi wa majengo ulioandaliwa na NEMC kwa kushirikiana na Kituo cha Sayansi na Mazingira cha Nchini India (CSE), Dkt.Jafo amesema uhifadhi na usimamizi wa mazingira ni mojawapo ya maeneo ya vipaumbele vilivyopo katika malengo makuu ya Serikali.
Dkt. Jafo amesema mwongozo ambao umezingatia mahitaji halisi ya nchi ikiwemo ukuaji wa miji na majiji, limeipa NEMC mamlaka ya kuhakikisha hali ya mazingira inaboreshwa nchini kwa kusaidia uboreshaji wa afya ya jamii ikiwa ni pamoja na mazingira vinalindwa na kuweka mazingira bora ya uwekezaji nchini.

‘’Kipengele Na. 17 cha Makubaliano ya Mkutano wa Umoja wa Mataifa kuhusu Maendeleo Endelevu unazitaka nchi wanachama kuhusisha tathmini za athari za mazingira katika miradi ambayo inasababisha madhara kimazingira…. katika kutekeleza kipengele hicho zilianzisha taasisi, na kutengeneza Sera na Sheria ikiwa ni pamoja na Kanuni kama ilivyo kwenye Kanuni ya Athari ya Mazingira za Mwaka 2005 na zile za Mwaka 2018,’’amesema Dkt.Jafo.
Kwa mujibu wa Waziri Jafo amesema, Tathmini za Athari kwa Mazingira (TAM) hufanyika ili kuweka mifumo bora ya kulinda mazingira ikiwa ni pamoja na kupunguza kiwango cha taka zinazozalishwa, kutoa kipaumbele katika masuala ya jamii, kuainisha athari zilizopo na madhara yanayoweza kujitokeza kutokana na miradi inayoanzishwa.

Waziri Jafo amesema NEMC inapokea zaidi ya miradi 2000 kwa mwaka kwa ajili ya mapitio na kuongeza kuwa idadi hiyo ya miradi ni kubwa na itaweza kupitiwa kwa ufanisi iwapo kutakuwa na miongozo ya kila sekta kama inavyoelekezwa katika Sheria ya Mazingira ya Mwaka 2004.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais, Mhe. Dkt. Selemani Jafo akimsikiliza Mkurugenzi wa Mradi wa Kituo Kituo cha Sayansi na Mazingira cha Nchini India (CSE) Bw. Nivit Yadav (anayezungumza) wakati wa hafla ya uzinduzi wa Mwongozo wa Ukaguzi wa Mazingira kwa Miradi ya Ujenzi wa Majengo baina ya NEMC na Kituo cha Sayansi na Mazingira, Nchini India (CSE). Hafla hiyo ilifanyika leo Jumatano (Oktoba 18, 2023) katika Mji wa Serikali, Mtumba Jijini Dodoma.

Dkt.Jafo ameishukuru Serikali ya India kupitia kituo hicho kwa kushirikiana na NEMC katika kuandaa mwongozo huo kwani ushirikiano huo ni ishara ya ya matokeo ya ushIrikiano wa taasisi hizo katika kupatia ufumbuzi wa changamoto za kimazingira.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Dkt.Selemani Jafo (kushoto) akibadilishana mawazo na Watendaji Waandamizi wa Kituo cha Kituo cha Sayansi na Mazingira cha Nchini India (CSE) kutoka kulia Shobhit Srivastava, Naibu Meneja Mkurugenzi na Bw. Nivit Yadav, Mkurugenzi wa Mradi muda mfupi baada ya uzinduzi wa mwongozo wa wa ukaguzi wa Mazingira kwa Miradi ya Ujenzi wa Majengo. Hafla hiyo ilifanyika katika Mji wa Serikali, Mtumba Jijini Dodoma leo Jumatano (Oktoba 18, 2023).

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Kituo cha Sayansi na Mazingira cha Nchini India (CSE),Nivit Yadav amesema Tanzania ni nchi ya tatu Bara la Afrika yenye kasi kubwa ya idadi ya watu na nchi ya pili kwa Mataifa ya Afrika Mashariki kuwa na kasi ya ukuaji wa sekta ya ujenzi, hivyo suala la tathmini ya miradi ya ujenzi ni jambo muhimu linalopaswa kupewa kipaumbele katika uhifadhi na usimamizi wa mazingira.

Amesema, Sheria ya Uhifadhi na Usimamizi wa Mazingira ya mwaka 2004 imeanisha vipaumbele mbalimbali vya utekelezaji wa Sheria hiyo ikiwemo kanuni na miongozo ya utekelezaji ikiwemo ushirikiano baina ya Serikali w ikiwemo NEMC na CSE.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Dkt. Selemani Jafo akiwa katika picha ya pamoja na na Watendaji na Viongozi wa Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) na Kituo cha Kituo cha Sayansi na Mazingira cha Nchini India (CSE) muda mfupi baada ya uzinduzi wa mwongozo.

Naye Mkurugenzi Mkuu wa Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC), Dkt. Samwel Gwamaka amesema kwa muda mrefu kumekuwepo na changamoto ya usimamizi wa tathmini ya athari kwa mazingira kupitia maandiko ya miradi mbalimbali yanayowasilishwa kwa ajili ya utoaji wa vibali vya mazingira.

“Awali wataalamu wetu hawakuwa na mwongozo wa maandiko ya tathmini ya miradi ya athari za mazingira ambayo inakidhi matakwa ya Sheria ya Usimamizi wa Mazingira na kanuni zake.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Dkt. Selemani Jafo akibadilishana mawazo na Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) Prof. Eng. Esnati O. Chaggu pamoja na Mkurugenzi Mkuu wa NEMC, Dkt. Samuel Gwamaka muda mfupi baada ya baada ya uzinduzi wa mwongozo wa wa ukaguzi wa Mazingira kwa Miradi ya Ujenzi wa Majengo. Hafla hiyo ilifanyika katika Mji wa Serikali, Mtumba Jijini Dodoma leo Jumatano (Oktoba 18, 2023).(PICHA NA OFISI YA MAKAMU WA RAIS).

"Baada ya uzinduzi huu sasa wataalamu elekezi wa mazingira na wadau watakuwa na mwongozo wa uaandaji wa maandiko kwa kuzingatia viwango na ubora unaohitajika,”amesema Dkt.Gwamaka.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news