Yanga yatinga hatua ya Makundi Ligi ya Mabingwa barani Afrika

DAR ES SALAAM-Klabu ya Yanga ya jijini Dar es Salaam imefanikiwa kutinga hatua ya makundi ya Ligi ya Mabingwa barani Afrika.

Ni baada ya ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Al Merreikh ya Sudan kupitia mtanange wa nguvu uliopigwa Septemba 30,2023 katika Dimba la Azam Complex lililopo Kata ya Chamazi ndani ya Halmashauri ya Manispaa ya Temeke.

Clement John Mzize dakika ya 66 kwa kichwa akiunganisha krosi ya beki Joyce Lomalisa Mutambala kutoka upande wa kushoto mwa dimba ndiye aliyewaandikia rekodi ya namna yake waajiri wake hao.

Mabingwa hao wa Ligi Kuu ya Tanzania Bara wanakwenda hatua ya 16 bora kwa ushindi wa jumla wa 3-0 kufuatia kuwachapa Al Merreikh 2-0 kwenye mchezo wa kwanza wiki mbili zilizopita jijini Kigali, Rwanda.

Yanga imeandika rekodi ya namna yake ikizingatiwa kuwa mara ya mwisho kwenda hatua ya makundi ya Ligi ya Mabingwa barani Afrika ilikuwa mwaka 1998.

Wanajangwani hao miaka hiyo waliwacharaza Rayon Sport ya nchini Rwanda na Coffee ya nchini Ethiopia katika raundi mbili za awali huku msimu huu wanafika hatua hiyo baada ya kuzitoa ASAS ya Djibouti na Al Merreikh ya Sudan.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news