Serikali yamaliza mgogoro wa ardhi kati ya wananchi na Chuo Kikuu cha Kilimo Katavi

KATAVI-Agizo la Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania,Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan la kumtaka Waziri mwenye dhamana ya ardhi kumaliza mgogoro wa ardhi kati ya wakazi wa Mtaa wa Rungwa Kata ya Kazima Mpanda Katavi na Chuo cha Kilimo Katavi (KUA) limefikia tamati baada ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Mheshimiwa Jerry Silaa kukabidhi hatimilki za ardhi kwa wananchi hao.

Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi,Jerry Silaa akisalimiana na wananchi mara baada ya zoezi la kukabidhi hati kwa wakazi wa Rungwa Kata ya Kazima Katavi Mpanda ikiwa ni hatua muhimu ya kumilikishwa ardhi baada ya kuisha kwa mgogoro wa ardhi kati ya wakazi hao na Chuo cha Kilimo Katavi.

Akiongea katika hafla fupi ya kukabidhi hatimilki za ardhi kwa wananchi hao, Waziri Jerry Silaa amesema, amefanikiwa kumaliza mgogoro huo kufuatia taarifa ya Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi,Daniel Chongolo kwa Rais Samia Suluhu Hassan alipohitimisha ziara yake mkoani Katavi, hivyo Rais kutoa agizo la kukamaliza mgogoro huo.

Waziri Silaa amebainisha kuwa, Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan alimuagiza kumaliza mgogoro huo kuisha kabisa baada ya kuwa amepata taarifa kutoka kwa viongozi wa mkoa na chama na kuongeza kuwa alimtaka kuhakikisha mwaka mpya ujao unaanza bila ya kuwa na mgogoro wowote.

‘’Nilikuja hapa tarehe 7 mwezi wa kumi mwaka huu na kutoa maagizo kwa Wizara ya Ardhi kuhakikisha inatekeleza maagizo ya Rais Dkt, Samia Suluhu Hassan kwamba mgogoro huu ufike mwisho na niwambie tangu nipate uteuzi na kupewa maelekezo ya nini kifanyike sijawai kukutana na mgogoro wa ardhi ambao hautatuliki,’’amesema Waziri wa Aedhi, Jerry Silaa.

Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Jerry Silaa akikabidhi hati kwa Bi. Fauzia Makoloka Abeid wakati wa zoezi la kukabidhi hati kwa wakazi wa Rungwa Kata ya Kazima Katavi Mpanda ikiwa ni hatua muhimu ya kumilikishwa ardhi baada ya kuisha kwa mgogoro wa ardhi kati ya wakazi hao na Chuo cha Kilimo Katavi.

Katika hatua nyingine Waziri Silaa ameagiza Uongozi wa Mkoa wa Katavi pamoja na wananchi kitongoji cha Rungwa kuhakikisha wanalinda maeneo 13 ya wazi,hospitali, masoko,makabuli na maeneo ya shule za awali pamoja na shule za msingi na sekondari.

Naye Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi Mkoa wa Katavi, Iddi Kimanta amebainisha kuwa kuna viongozi wengi mkoani Katavi ambao kwa kipindi kirefu waliangaika na mgogoro huu bila mafanikio lakini jana Waziri mwenye dhamana ya ardhi alifanikiwa kumaliza mgogoro huo.

Kufuatilia hali hiyo Mwenyekiti huyo wa CCM mkoa wa Katavi alimtaja Waziri mwenye dhamana ya Ardhi Jerry Silaa kuwa anaingia kwenye historia kwa kufanikiwa kumaliza mgogoro huo.

Bw. Iddi Kimanta aliongeza kuwa taarifa za Chama na Serikali wakati wa ziara ya Katibu Mkuu wa Chama mkoani Katavi taarifa zote zilitaja mgogoro huu na katika taarifa zote hizo walimuomba kuhakikisha anakomesha mgogoro huo ambao ulikuwa na maslahi mapana ya wananchi.

Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Jerry Silaa akikabidhi hati kwa Mkazi wa Rungwa Kata ya Kazima Katavi Mpanda ikiwa ni hatua muhimu ya kumilikishwa ardhi baada ya kuisha kwa mgogoro wa ardhi kati ya wakazi hao na Chuo cha Kilimo Katavi.

Naye Mkuu wa Wilaya ya Mpanda Bi.Jamila Yusufu amehaidi kuwa, kwa kuwa mgogoro huu umekwisha basi hawatakubali kuona unazalisha mgogoro mwingine kwenye neo hili maarufu KUA.

"Tutasimamia kikamilifu, tutasimamia sheria kikamilifu,kuhakikisha eneo hili halizalishi migogoro ten ana niwaombe wananchi shukrani pekee ambayo tunaweza kumpa Mhe. Rais ni kutozalisha mgogoro mwingine katika eneo hili tena."

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news