Tanzania kunufaika kupitia IDA20 Mid Term Review utakaofanyika Zanzibar

ZANZIBAR-Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inatarajia kunufaika na Mkutano wa Kimataifa wa Tathimini ya Muda wa Kati wa Mzunguko wa 20 wa Benki ya Dunia (IDA20 Mid Term Review) utakaofanyika Zanzibar kuanzia tarehe 6 hadi 8 Desemba, 2023, ukiwashirikisha wajumbe zaidi ya 300 kutoka mataifa takribani 100 duniani.
Hayo yamebainishwa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Fedha na Mipango-Zanzibar, Mheshimiwa Dkt. Saada Mkuya Salum, wakati akifungua kikao cha Kamati ya Maandalizi ya Mkutano huo, kilichofanyika katika Ukumbi wa Mikutano Wa Wizara ya Fedha na Mipango, Unguja-Zanzibar.

Alisema kuwa mkutano huo ni muhimu kwa maendeleo ya nchi 75 wanachama wa Taasisi hiyo ya Benki ya Dunia ikiwemo Tanzania, ambapo masuala kadhaa yatajadiliwa kuhusu fursa na changamoto zinazotokana na kukabiliana na umasikini.

Mhe. Dkt. Saada Mkuya Salum alisema kuwa, Tanzania ni mdau mkubwa wa Benki ya Dunia na kwamba mkutano huo utatoa fursa ya wajumbe watakaohudhiria kujionea maendeleo makubwa ya nchi yaliyopatikana kutokana na mikopo nafuu, misaada na ushauri wa kiufundi unaotolewa na Taasisi hiyo kubwa ya fedha duniani.

Aliitaka Kamati hiyo kuhakikisha kuwa mkutano huo unaandaliwa kwa viwango vya kimataifa ili kuitangaza Tanzania katika medani za kimataifa kwa uwezo wake wa kuandaa mikutano ya namna hiyo hatua itakayovutia wageni wengi zaidi kufanya mikutano kama hiyo hapa nchini na kuinufaisha Serikali na wananchi kwa ujumla.

Kwa upande wake, Mjumbe wa Kamati hiyo, ambaye pia ni Katibu Mkuu wa Wizara ya Uchumi wa Buluu na Uvuvi, Dkt. Aboud Suleiman Jumbe, alisema kuwa Benki ya Dunia imeisadia Tanzania katika nyanja za kiuchumi ikiwemo Sekta ya Uchumi wa Buluu Viwani Zanzibar.

Alisema kuwa ni matarajio yake kwamba mkutano huo utakaowashirikisha Rais wa Benki ya Dunia, Bw. Ajay Banga, Viongozi Waandamizi wa Benki ya Dunia, wawakilishi wa nchi zinazonufaika wa IDA, pamoja na wafadhili wanaochangia fedha katika dirisha la IDA, utakuwa na manufaa kwa wananchi na Serikali kwa ujumla.

Benki ya Dunia inatumia takribani theluthi tatu ya fedha kwa ajili ya kuzisaidia nchi zinazoendelea zilizopo Kusini mwa Jangwa la Sahara kutekeleza miradi mbalimbali ya kimkakati ambayo lengo lake ni kukabiliana na umasikini na mkutano utakaofanyika Zanzibar utatoa fursa kwa nchi wanachama kutafakari mafanikio na changamoto za mfuko huo.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news