Wafanyakazi michango yenu ya WCF huwa inapelekwa wapi?

NA GODFREY NNKO

MFUKO wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF) umeendelea kurejesha tabasamu kwa maelfu ya wafanyakazi wanaopata madhila kila siku wakiwa kazini nchini.
Hayo yamebainishwa Novemba 2, 2023 jijini Dar es Salaam na Mkurugenzi Mkuu wa mfuko huo,Dkt.John Mduma katika kikao kazi kati ya wahariri wa vyombo vya habari nchini chini ya uratibu wa Ofisi ya Msajili wa Hazina.

Dkt.Mduma amesema, wajibu mkuu wa WCF ni kulipa fidia stahiki kwa wafanyakazi wanaopata ajali au ugonjwa unaotokana na kazi na kwa wategemezi wa wafanyakazi wanaofariki dunia kutokana na kazi.

Katika kutekeleza hili, Dkt.Mduma amesema WCF inalinda nguvu kazi ya Taifa, kupunguza umaskini, kusaidia kuondoa migogoro kati ya waajiri na wafanyakazi hasa pale mfanyakazi anapopata ajali au ugonjwa unaotokana na kazi.

Mbali na hayo, WCF inawezesha waajiri kutekeleza majukumu yao ya uzalishaji badala ya kushughulikia madai ya fidia ikiwemo kusaidia kuleta uelewano na utulivu katika jamii.

Amesema, hadi Septemba 2023 shilingi bilioni 65.34 zimelipwa huku jumla ya madai 18,782 yakiwa yamepokelewa kati ya madai hayo 14,087 yameshughulikiwa huku 12,339 yakilipwa, madai 1,440 yalikataliwa na 308 yamefungwa.

Vile vile, waliopo katika pensheni ya shilingi milioni 413 ni 1,466, wanaohitaji wasaidizi ni 18, ulemavu zaidi ya asilimia 30 ni 358, wategemezi ni 1,090 na wanafunzi ni 26.

Amesema, kwa sasa mfuko huo unatoa mafao saba ikiwemo Fao la Matibabu, Fao la Ulemavu wa Muda, Fao la Ulemavu wa Kudumu,Fao la Kumuuguza Mgonjwa,Malipo Kwa Wategemezi,Msaada wa Mazishi na Fao la Utengemao.

Pia, amesema kupitia Mafao ya Utengamao (rehabilitation) wanatoa utengamao wa matibabu, kijamii na utengemao wa ujuzi. "Lengo ni kuondoa umasikini wa kipato, kulinda nguvu kazi ya Taifa na kuleta utulivu katika jamii."

Akizungumzia kuhusu Mafao ya Wategemezi, Dkt.Mduma anasema, hulipwa kwa ngazi ukianza na mweza,watoto au wazazi ambapo mwenza hulipwa asilimia 40 ya mshahara ghafi kwa maisha yake yote.

Pia,anabainisha kuwa, kiwango cha chini ni shilingi 110,281.13 kwa mwezi."Watoto hulipwa asilimia 20, hubadilika watoto wanapozidi watatu na malipo ni mpaka watimize miaka 18 au kualiza elimu ya sekondari au chuo.

"Kwa hiyo, WCF tunapunguza umasikini, tunaondoa migogoro, tunaleta utulivu, tunaongeza ari ya kazi na mahusiano bora kazini,"amefafanua Dkt.Mduma.

Kuhusu Mafao ya Anayemhudumia Mgonjwa anasema,hulipwa kwa mfanyakazi asiyeweza kumudu kujihudumia ambapo ni asilimia 40 ya pensheni ya mfanyakazi.

Anafafanua kuwa, msaidizi huteuliwa na mfanyakazi huku dhamira ikiwa ni ile ile ya kuondoa migogoro kati ya waajiri na wafanyakazi ikiwemo kuleta utulivu katika jamii.

Mafao ya Ulemavu wa Kudumu anasema, haya hulipwa asilimia 70 ya mshahara ghafi mara kiwango cha ulemavu ambapo kiwango cha chini ni shilingi 275,702.83.

Dkt.Mduma anafafanua kuwa, ulemavu usiozidi asilimia 30 hulipwa kwa mkupuo huku ulemavu unaozidi asilimia 30 hulipwa kwa pensheni kwa maisha yote ambapo wanaendelea kutoa uhakika wa kipato endelevu kwa mfanyakazi.

Amesema, kwa upande wa Mafao ya Matibabu huanza kulipwa mara ajali inapotokea ambapo aina zote za matibabu hutolewa bila kujali kiwango cha uchangiaji.

"Mfumo wote wa matibabu Tanzania Bara (bima na watoa huduma za afya) hutoa huduma kwa wateja wa WCF, hakuna ukomo wa gharama za matibabu na hakuna kifurushi cha matibabu."

Katika hatua nyingine, Dkt.Mduma anasema,thamani ya mfuko huo hadi kufikia Septemba, mwaka huu ilikuwa shilingi bilioni 697.5.Pia, mapato ambayo yanatokana na uwekezaji wa mfuko yanafikia zaidi ya shilingi bilioni 300.

Dkt.Mduma anafafanua kuwa, vyanzo vya mapato vya mfuko huo ni michango toka kwa waajiri, fedha zinazolipwa na waajiri kutokana na adhabu ya kuchelewa kulipa michango kwa wakati,mapato yatokanayo na shughuli za uwekezaji.

Vyanzo vingine ni gawio toka serikalini yakiwemo mapato mengine yoyote halali yanayopatikana kutokana na shughuli mbalimbali za mfuko.

Dkt.Mduma amesema, wakati mfuko unaanza mwaka 2015 waliweza kusajili asilimia 15 ya waajiri ambao walikuwa 5,178 katika database yao, lakini hadi kufikia Septemba mwaka huu usajili umefikia zaidi ya asilimia 93 sawa na waajiri 31,469.

"Mfuko wa Fidia kwa Wafayakazi (WCF) ni Taasisi ya Hifadhi ya Jamii iliyoundwa kwa mujibu wa Sheria ya Fidia kwa Wafanyakazi Sura 263. Mfuko ulianza rasmi Julai 1, 2015 na kupewa mwaka mmoja (grace period) kabla ya kuanza rasmi ulipaji wa mafao ya fidia kwa walengwa.

"Lengo la kipindi hicho lilikuwa ni kuuwezesha mfuko kuwa na rasilimali fedha zinazohitajika kulipa fidia kwa walengwa.Majukumu mengine yote yaliendelea kutekelezwa ikiwemo usajili wa waajiri na ukusanyaji wa michango."

Sababu

Dkt.Mduma anasema, sababu za kuanzishwa kwa WCF ni baada ya Serikali kubaini changamoto mbalimbali ambazo zilikuwa zinawakabili wafanyakazi huku sheria ya awali ikionekana kuwa na mapungufu.

"Tanzania, kama ilivyo kwa nchini nyingi za kiafrika, ilirithi sheria nyingi kutoka kwa wakoloni baada ya kupata uhuru. Moja ya sheria iliyorithiwa kutoka kwa Waingereza ilikuwa ni sheria ya fidia kwa wafanyakazi ya mwaka 1949 (The Workmen’s Compensation Ordinance).

"Sheria hii iliweka jukumu la kulipa fidia kwa mwajiri. Gharama za kumtibu mfanyakazi aliyeumia zilibebwa na mwajiri. Ukomo wa fidia iliyolipwa kwa wafanyakazi waliopata ulemavu kutokana na ajali ilikuwa ni shilingi 108,000.00 na iwapo mfanyakazi angefariki, familia yake ingelipwa shilingi 83,333.33.

"Malipo ya fidia yalikuwa ni ya mkupuo isipokuwa kwa makubaliano kati ya mwajiri na mfanyakazi au kwa amri ya mahakama.

"Changamoto nyingine za sheria hiyo zilikuwa ni pamoja na kupitwa na wakati kwa Sheria husika na marekebisho mengi,viwango vidogo vinavyolipwa chini ya sheria hiyo.

"Kukosekana kwa haki ya fidia pale mwajiri anapokuwa amefunga biashara,mlolongo mrefu wa kupata fidia uliohusisha mahakama hasa pale mfanyakazi anapopata magonjwa yanayotokana na kazi na sheria kutokulinda wafanyakazi pale wanapopata ajali wakienda au kurudi kazini,"amefafanua Dkt.Mduma.

Anasema kuwa,sheria ya WCF inawahusu waajiri na waajiriwa wote katika sekta rasmi Tanzania Bara ingawa haifanyi kazi kwa wafanyakazi walioajiriwa kwenye sekta isiyo rasmi.

Pia, mfanyakazi aliyeajiriwa au kufanyakazi kwa siku pungufu ya 30 mfululizo ikijumuishwa na siku za mapumziko za kitaifa na siku za Jumamosi na Jumapili.

Faida

Dkt.Mduma anasema, kuna faida nyingi za WCF ikiwemo uhakika wa muendelezo wa kipato kwa mfanyakazi aliyepata ulemavu wa kudumu na kushindwa kurudi kazini.

Faida nyingine,Dkt.Mduma anasema ni kupunguza umaskini hususani kwa wategemezi na wafanyakazi wanaopata
ulemavu wa kudumu na kushindwa kurudi kazini au kufariki.

"Kupitia sisi, tunawezesha uwepo wa mazingira bora kazini kutokana na mahusiano mazuri kati ya mwajiri na mwajiriwa, malipo mazuri ya fidia na hivyo kuongezeka kwa motisha kwa wafanyakazi

"Pia, tunasaidia kupungua kwa malalamiko na migogoro baina ya waajiri na wafanyakazi sehemu za kazi hali ambayo kabla ya kuanza kwa WCF ilikuwa inasababishwa na mwajiri kuchelewa kulipa fidia au kulipa fidia kidogo,"anasisitiza Dkt.Mduma.

Vile vile, Mkurugenzi Mkuu huyo anasema, uwepo wa WCF unawezesha waajiri kuwa na muda mrefu wa kuendelea na kazi za uzalishaji na ongezeko la tija kazini kutokana na mahusiano mazuri kati ya waajiri na waajiriwa.

"Faida nyingine ni kuchangia ongezeko la uzalishaji na maendeleo ya Taifa kupitia ongezeko la tija, ongezeko la pato la taifa na kodi ili kuiwezesha Serikali kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi,"anabainisha Dkt.Mduma.

Mbali na hayo, Dkt.Mduma amesema, wamefanikiwa kuboresha huduma kupitia usimikaji mifumo ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA),kuboresha kwa kituo cha huduma kwa wateja na kuboresha tathmini za ulemavu kupitia mafunzo kwa madaktari.

Michango

Kwa upande wa ukusanyaji michango, Dkt.Mduma amesema, waajiri wote wanatakiwa kuchangia katika mfuko ambapo waajiri sekta binafsi ni asilimia 0.5 na waajiri sekta ya umma ni asilimia 0.5.

"Serikali ya awamu ya Sita chini ya Mhe. Dk. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imefanya maboresho mbalimbali ikiwemo kupunguzwa kwa kiwango cha uchangiaji kwa waajiri wa sekta binafsi kutoka kiwango cha asilimia moja ya awali hadi kufikia asilimia sifuri nukta tano."

Maboresho mengine amesema ni kupunguzwa kwa riba kwa waajiri waliochelewesha michango kutoka asilimia 10
iliyokuwa ikitozwa kwa mwezi hadi kufikia asilimia 2 ya sasa.

"Kufutiwa riba ya malimbikizo ya michango kwa waajiri waliochelewa kulipa na kuongezwa kwa kima cha chini cha fidia kutoka utaratibu wa awali ambao haukuwa na kima cha chini cha fidia kwa mfanyakazi ambaye hakupata ulemavu wa asilimia 100 hadi kufikia shilingi 275,702.83 za sasa."

Uwekezaji

Dkt.Mduma anasema kuwa, mfuko huo unaendelea na uwekezaji wa kimkakati katika kufufua kiwanda cha chai cha Mponde.

Amesema, WCF kwa kushirikiana na PSSSF pamoja na Ofisi ya Msajili wa Hazina imeunda kampuni ya Mponde Holding Company Limited inayoendesha kiwanda cha chai cha Mponde.

"Mchakato wa ufufuaji wa kiwanda hicho umekamilika na kiwanda kilianza uzalishaji wa kibiashara mwezi Oktoba 2022.Aidha, kiwanda kimekuwa na mchango mkubwa katika sekta ya uchumi ikiwemo uzalishaji wa chai,ajira zaidi ya 1,181 kwa wakulima na vibarua 110."

Uimara

Dkt.Mduma anasema,uimara wa WCF kwa tathmini ya Shirika la Kazi Duniani (ILO) ni mkubwa. "Kwa mujibu wa ripoti ya tathmini ya mfuko (actuarial valuation) iliyofanywa na ILO mwaka 2018. Mfuko wa WCF ni imara na unauwezo wa kutekeleza majukumu yake bila kutetereka.

"Matokeo ya tathmini hiyo pia yalipendekeza kupunguzwa kwa viwango vya uchangiaji ambapo Serikali ilitekeleza kuanzia mwaka wa fedha 2021/22."

Aidha, Dkt.Mduma amesema, WCF imefanya tathmini ya pili mwaka 2022 na ambayo imeonesha kuwa Mfuko wa WCF bado ni himilivu na unauwezo wa kuendelea kutoa huduma bila wasiwasi kwa kipindi cha miaka 30 ya tathmini (2022/23-2051/52).

Wanufaika

Beauty Jackson Letema ambaye ni mke wa marehemu Michael Gready Lameck amekuwa akinufaika na fidia inayotolewa na mfuko huo tangu mume wake afariki akiwa kazini na amekuwa akipata huduma bora kutoka WCF.

Lameck ambaye alifariki kwa ajali ya kugongwa na mashine ya kunyanyulia makasha akiwa kazini Desemba, 2021 aliwaacha mke na watoto ambao ni wategemezi Sarah, Noel, Nathaniel na Nachman

“Ninamshukuru sana Mwenyezi Mungu, lakini pia naishukuru WCF, mume wangu alipofariki aliniacha na watoto watatu na ujauzito.

"WCF walianza kunihudumia mimi na watoto wangu hao watatu na kisha huyu mwingine. Mimi sikuwa na kazi yoyote ya kufanya, WCF wanatuhudumia mimi na watoto, tunavaa, tunakula na pia watoto wangu wanasoma bila shaka yoyote, kwa kweli wamenifuta machozi,”amesema Beauty ambaye ni mama wa watoto wanne.

Mama huyo amewahimiza waajiri kujisajili na mfuko ili wafanyakazi wanapopatwa na madhila wakiwa kazini, basi mfuko utakuwa mfariji wao kuanzia mwanzo wa safari hadi mwisho.

“Wito wangu kwa waajiri, WCF ni mfuko wenye faida sana, kama mimi mume wangu alivyofariki na mwajiri wake angekuwa hajajisajili WCF, maisha yangekuaje? Natoa wito kwa waajiri wajiunge na WCF.”

Mnufaika mwingine, Hassan Sima Jambau ambaye alipata ajali ya pikipiki Februari 1,2018 na kukatika mguu wa kulia chini ya goti amesema, WCF ilikuwa faraja katika kipindi chote kigumu ambacho alikuwa anapitia.

“Kwa kifupi naishukuru sana Serikali kwa kuanzisha WCF. Mfuko una manufaa makubwa sana, ninajitegeema asilimia 100, namshukuru Mkurugenzi Mkuu wa WCF na timu yake. Mfuko umenipatia matibabu vizuri sana hadi kupona, maisha yangu yanaendelea.”

Jambau alipatiwa na WCF matibabu yote mpaka kufikia MMI,huduma ya utengemao wa kimatibabu kwa kupewa kiungo bandia (clinical rehabilitation) na mafao ya ulemavu wa muda na kudumu huku akiendelea kupata pensgeni ya kila mwezi kwa maisha yake yote.

Naye Halima Sheikh Mbwana ambaye alipata ajali Mei, 2022 huku akiumia kutokana na ajali akiwa anaendesha basi la abiria la Super Feo kutokea Songea kwenda Dar es Salaam alisema,alikatika mkono wa kulia baada ya basi ambalo alikuwa anaendesha kupinduka.

“Baada ya kupoteza mkono na kupata ulemavu wa kudumu, WCF imekuwa ikinilipa fidia kila mwezi, malipo yananisaidia mimi na familia yangu, nimeambiwa nitalipwa maisha yangu yote, hakika nafarijika sana.”

Kwa mujibu wa WCF, Halima alipata matibabu yote kwa mujibu wa sheria ikiwemo huduma ya utengemao wa kimatibabu (clinical rehabilitation na mafao ya Ulemavu wa Muda na Kudumu.

Mbali na hayo, WCF inafafanua kuwa,viwango vya malipo ya pensheni vitakuwa vinarejewa mara kwa mara kulinda thamani ya malipo.

TR

Akizungumza katika kikao kazi hicho,Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Ofisi ya Msajili wa Hazina, Thobias Makoba amewaomba wanahabari kuendelea kushirikiana na Serikali kwa ajili ya kuhabarisha umma kuhusu mambo mbalimbali yanayofanyika nchini.

Amesema, Serikali inatekeleza miradi mingi ikiwemo ya kimkakati ambayo inahitaji ushirikiano wa vyombo vya habari ili umma uweze kutambua yanayofanyika.

“Kuna mambo mengi mazuri ambayo Mheshimiwa Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan anayafanya, kupitia miradi na mageuzi haya ya kiuchumi yanatakiwa umma uweze kufahamu kupitia vyombo vyenu vya habari."

Wakati huo huo, Dkt.Mduma ameipongeza Ofisi ya Msajili wa Hazina chini ya Msajili wa Hazina, Nehemiah Mchechu kwa kuja na ubunifu huo ambao unawezesha umma kufahamu yale ambayo yanafanywa na taasisi na mashirika yao, yalikotoka, yalipo na yanapokwenda. "Ninampongeza sana Msajili wa Hazina, mwambieni ofisi yetu hii ina afya tele."

TEF

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF), Deodatius Balile amewataka wanahabari kwenda kuwaeleza waajiri wao umuhimu wa kuwasajili WCF.

"Nendeni mkaidai hii haki ya kusajiliwa WCF kwa waajiri wenu. Ni suala la uamuzi, wala halihitaji gharama yoyote."

Pia, Balile ameendelea kuipongeza Ofisi ya Msajili wa Hazina kwa namna ambavyo imekuwa mstari wa mbele katika kuviunganisha vyombo vya habari na taasisi za umma ili ziweze kuelezea yale ambayo wanayatekeleza kwa manufaa ya umma.

Vile vile, ameipongeza WSF kwa kuendelea kuwa mdau muhimu katika jukwaa hilo na vyombo vya habari kwa ujumla nchini.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news