Serikali yaahidi kuendeleza ushirikiano na IMF kuhakikisha ukuaji endelevu wa uchumi

DAR ES SALAAM-Waziri wa Fedha, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Nchemba na Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania, Bw. Emmanuel Tutuba, wamelihakikishia Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF) kwamba Tanzania itaendelea kushirikiana na IMF katika kuhakikisha ukuaji endelevu ya uchumi wa nchi.

Ahadi hiyo imetolewa na Waziri wa Fedha, Dkt. Mwigulu Nchemba, na Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania, Bw. Emmanuel Tutuba, katika kikao cha kuhitimisha mapitio ya pili ya mpango wa miezi 40 wa ukopeshaji wa ECF kati ya Serikali na ujumbe wa IMF, kilichofanyika tarehe 03 Novemba, 2023, katika Ofisi Ndogo za Makao Makuu ya Benki Kuu ya Tanzania Dar es Salaam.
Mhe. Dkt. Mwigulu, ambaye alishiriki kikao hicho kwa njia ya mtandao, alielezea dhamira ya Serikali ya kushirikiana kwa karibu na IMF kwa ajili ya kuimarisha uhimilivu na ushirikiano katika sekta ya fedha.

Pia, Gavana Tutuba alisisitiza matarajio ya Benki Kuu kuhama kutoka kutumia Mfumo wa Sera Ya Fedha unaolenga Ujazi wa Fedha kwenda Mfumo wa Utekelezaji wa Sera ya Fedha Unaotumia Riba kwa lengo la kuimarisha uchumi wa nchi.

Ujumbe wa IMF, ukiongozwa na Bw. Charalambos Tsangirides, ambaye ni Mwakilishi wa IMF hapa Tanzania, ulifanya mikutano na Serikali Dodoma na Dar es Salaam kuanzia Oktoba 23 hadi Novemba 3,2023, ili kujadili maendeleo ya mageuzi na vipaumbele vya sera za Serikali katika muktadha wa mapitio ya pili ya mpango wa ukopeshaji wa ECF.

Bw. Tsangirides alipongeza jitihada zinazofanywa na serikali katika kusimamia uchumi wa nchi pamoja na uwepo wa changamoto zinazoukumba uchumi wa dunia.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news