Rais Dkt.Samia atia saini Muswada wa Sheria ya Bima ya Afya kwa Wote

NA DIRAMAKINI

RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt.Samia Suluhu Hassan ametia saini Muswada wa Sheria ya Bima ya Afya kwa wote na sasa imekuwa sheria kamili.
Mheshimiwa Rais amefanya hivyo ikiwa Novemba 2, 2023 Muswada wa Sheria ya Bima ya Afya kwa Wote ulipita kwa kishindo baada ya Bunge kuupitisha kwa asilimia 100 na kutangazwa kupitia Gazeti la Serikali Desemba 1, 2023.

Aidha, unatajwa kwenda kuweka historia kwa Serikali ya Awamu ya Sita kwa kuuhakikishia umma juu ya huduma za matibabu kwa kundi la wananchi wasio na uwezo.

Wakati akiongea baada ya kupitishwa kwa muswada Spika wa Bunge, Mhe. Dkt. Tulia Akson aliipongeza Serikali kwa hatua hiyo na kuongeza kuwa sheria hiyo itakua mwarobaini kwa wananchi kupata huduma bora za afya.

Muswada wa Sheria ya Bima ya Afya uliwasilishwa bungeni jijini Dodoma na Waziri wa Afya, Mhe. Ummy Mwalimu ambapo alisema kupitia sheria hiyo kutakuwa na utaratibu wa utambuzi na usajili wa kundi la watu wasio na uwezo kwa lengo la kuhakikisha wanapata huduma za afya bila kikwazo cha fedha kwa utaratibu utakaowekwa na Serikali.

Kundi hilo litajumuishwa kwenye Skimu ya Bima ya Afya ya Umma kwa namna itakavyoainishwa kwenye kanuni zitakazotengenezwa hapo baadae huku akibainisha vyanzo vya mapato vitakavyotumika kugharamia skimu hiyo.

“Vyanzo vya mapato ya skimu hii ni pamoja na sehemu ya mapato yatokanayo na ushuru wa bidhaa kwenye vinywaji vyenye kaboni (carbonated drinks), Vinywaji vikali (Liqour), bidhaa za vipodozi (Cosmetic Products), Kodi ya michezo ya kubahatisha, ada ya bima za vyombo vya moto na mapato yatokanayo na ushuru wa miamala ya kielektroniki (Eletronic Transaction Levy) kwa kadri itakavyopendekezwa,”alisema Mhe. Waziri Ummy.

Kutokana na hayo, Mhe. Ummy alitumia mwanya huo kumshukuru na kumpongeza Rais wa Jamhuri wa Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa uamuzi wake wa kuhakikisha kuwa watu wasio na uwezo wanapata huduma bora za afya bila kikwazo chochote.

“Hakika historia ya Tanzania na Dunia itamkumbuka Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan pamoja na Spika Dkt. Tulia Ackson. Kipekee tunaishukuru Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Afya na masuala ya UKIMWI, kwa kuweka msisitizo wa umuhimu wa kuwa na mfuko kwa ajili ya kugharamia bima ya afya kwa watu wasio na uwezo na hili tutalisimamia kikamilifu kwa kuwa ni wajibu wa Serikali kuhakikisha kila wananchi anapata huduma bora za afya."

Hatua hiyo, sasa inatoa idhini kwa Waziri wa Afya kutunga kanuni zitakazowezesha utekelezaji wa sheria hiyo inayotaka kila Mtanzania kuwa na Bima ya Afya nchini.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news