Wazalishaji wa saruji watakiwa kuongeza uzalishaji kwa wingi na bora

DAR ES SALAAM-Waziri wa Viwanda na Biashara Mhe Dkt. Ashatu Kijaji (Mb.) amesema lengo la Serikali ya Awamu ya Sita ni kuona Viwanda vya Saruji nchini vinazalisha saruji kwa ubora na viwango vya kimataifa ili iweze kukidhi mahitaji na ushindani wa soko la ndani na nje ya nchi.
Vilevile Waziri Kijaji amewaahidi Wazalishaji hao wa saruji kuwa Serikali inaendelea kutatua changamoto mbalimbali wanazokabiliana nazo ikiwemo miundombinu ya umeme, barabara na maji ili kuboresha uzalishaji wa viwanda vya saruji nchini.

Amesema hayo Disemba 11, 2023 katika Kikao cha Wazalishaji wa Saruji nchini kilichofanyika Jijini Dar es Salaam ikiwa ni muendelezo wa kukutana kila baada ya miezi mitatu ili kusikiliza na kutatua Changamoto zinazowakabili ili kuongeza uzalishaji wa saruji wenye tija.
Aidha, Dkt. Kijaji amewashauri wazalishaji hao kuzalisha saruji yenye ubora na ili Saruji ya Tanzania iweze kuingia katika Soko la Eneo Huru la Biashara Afrika (AfCFTA) kutokana na ukubwa wa soko hilo lenye wateja zaidi ya bilioni 1.3.

Aidha, Dkt. Kijaji amebainisha kuwa hadi sasa uzalishaji wa saruji nchini ni tani milioni 11 kwa mwaka, mahitaji ya ndani ni takriban tani milioni 7.5. na ziada huuzwa nje ya nchi.
Naye Mwenyekiti wa Shirikisho la wenye Viwanda Tanzania (CTI), Bw Leodga Tenga ameiomba Serikali kuendelea kuboresha mazingira bora kwa wawekezaji na wafanyabiashara huku akiwashauri wamiliki hao wa Viwanda kuzalisha saruji yenye ubora kwa wingi ili kiweza kushindana katika soko la ndani na nje.
Naye Mkurugenzi wa Kiwanda cha Saruji Tanga Tanzania na Mjumbe wa Bodi ya CTI Mhandisi Benedict Lema ameishukuru Serikali kwa kuendelea kutatua changamoto mbalimbali na amesema kwa niaba ya wamiliki wa viwanda hivyo wapo tayari kushirikiana na Serikali katika kutatua changamoto mbali mbali ili kuweza kuboresha uzalishaji wa saruji nchini.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news