Yanga SC, Al Ahly SC watoana jasho kwa bao 1-1

DAR ES SALAAM-Mabingwa wa Ligi Kuu ya NBC Tanzania Bara, Klabu ya Yanga ya jijini Dar es Salaam wameshindwa kuonesha makali yao katika Ligi ya Mabingwa barani Afrika.

Ni baada ya wenyeji hao leo Desemba 2, 2023 kulazimishwa sare ya kufungana bao 1-1 na mabingwa watetezi,Al Ahly SC.

Mtanange huo wa Kundi D umepigwa leo Desemba 2, 2023 katika Dimba la Benjamin Mkapa lililopo Halmashauri ya Manispaa ya Temeke jijini Dar es Salaam.


Si Yanga SC wala wageni katika kipindi cha kwanza walienda mapumziko bila kufungana na kipindi cha pili kilianza kwa kila mmoja kufanya mabadiliko kwa ajili ya kusaka ushindi.

Klabu ya Al Ahly ilipata bao dakika ya 86 ambalo lilifungwa na Percy Muzi Tau. Lilikuwa ni bao ambalo lilianza kusababisha furaha ya mashabiki kuvurugika, lakini katika dakika ya 90+ Yanga SC ilizamisha jahazi.

Mwajiriwa wao kutoka nchini Ivory Coast, Kiungo Pacôme Zouzoua ndiye alisawazisha bao hilo, hivyo kurejesha tabasamu kidogo kwa mashabiki wa Yanga na Watanzania kwa ujumla.

Aidha, kwa matokeo hayo Al Ahly SC imefikisha alama nne na kuendelea kuongoza Kundi D kwa alama moja zaidi ya CR Belouizdad ya Algeria na Medeama ya Ghana.

Kwa upande wa Yanga SC sasa inaburuza mkia kwa alama moja baafa ya kupiga mechi mbili ambapo sasa Yanga SC itasafiri hadi nchini Ghana kucheza na Medeam siku ya Desemba 8, wakati Al Ahly SC watawakaribisha CR Belouizdad jijini Cairo nchini Misri.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news