Mwinjilisti Temba amtabiria makubwa Makonda, atoa onyo kwa wanaotaka kumshusha chini

DAR ES SALAAM-Muhubiri na Mwinjilisti wa Kimataifa, Alphonce Temba, watu wengi wanaomfuatilia mamia kwa maelfu wameendelea kutoa maoni na mawazo yao juu yake wakisema kwamba mtumishi huyu wa Mungu ni mtu ambaye amekuwa na maono makubwa kwa Taifa lake.
Muhubiri na Mwinjilisti wa Kimataifa Alphonce Temba (wa kwanza kulia) akiwa na Katibu wa NEC, Itikadi, Uenezi na Mafunzo wa Chama cha Mapinduzi (CCM) Paul Makonda. (Picha na Maktaba).

Wanasema kuwa Mtumishi huyu wa Mungu amekuwa ni Mzalendo wa kweli anayependa nchi yake, msema kweli na mjasiri katika karne ya sasa ambayo watu kama hawa wanahitajika.

"Huko nyuma kumekuwa na watumishi mbalimbali katika mataifa mbalimbali Duniani ambao wamefanya mambo makubwa akiwemo Desmond Tutu aliyekuwa Askofu wa Kanisa la Angilikana nchini Afrika Kusini, ambaye ni mmoja wapo aliyepaza kelele juu ya ubaguzi wa rangi katika nchi ya Afrika Kusini na kupambania uhuru wa Afrika Kusini kwa kupiga kelele na kuendelea kuwapinga Mabepari waliokuwa wakilitesa Taifa hilo kwa kugawa weupe na weusi. Watumishi wengine ni Yohana wa Pili pamoja na Masheikh mbalimbali wa Kimataifa Duniani ambao majina yao yaliibuka katika kutetea haki," wanasema watu hao wanaomfuatilia Mwinjilisti wa Kimataifa Temba na kuongeza,

"Na Tanzania wapo watumishi mbalimbali ambao wamekuwa mstari wa mbele kulipigania Taifa akiwemo Hayati Mchungaji Christopher Mtikila ambaye pamoja na kwamba alikuwa Mchungaji na Mwenyekiti wa Chama cha Democtratic Party (DP) aliibuka kutetea haki za Taifa na uzalendo wake hususan pale alipojikita kung'ang'ania uzalendo wa kutaka Chama chake kisajiliwe kama Chama cha Tanganyika. Kitendo hicho kilileta mvutano mkubwa kwa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) na Msajili wa Vyama vya Siasa na kilisajiliwa tu baada ya kukubali muungano na upande wa Tanzania Zanzibar."

Hata hivyo wanasema Mchungaji Mtikila aliendelea kupambana na kesi nyingi ambapo zipo zilizomuweka ndani na nyingine kuachiwa baada ya kukata rufaa ikiwepo kesi maarufu ambayo aliipambania mpaka dakika ya mwisho pasipo watu wengi kuiunga mkono kwani walidai anatafuta umaarufu.

"Kesi hiyo ni kesi ya mgombea binafsi, ambayo aliipambania katika Mahakama zote mpaka kufika katika Mahakama ya Afrika Mashariki, ikatoa mapendekezo yake na hukumu kwamba inapaswa mgombea binafsi aingizwe katika Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,".

Hivyo watu hao wanaomfuatilia Mwinjilisti Temba wanasema amekuwa akisifika kwa makala zake hususan katika kipindi hiki ambacho wanahitaji watu Mungu.

Wengine wamekuwa wakishangaa ni kwa namna gani Serikali ya Chama cha Mapinduzi (CCM) ambayo na yeye ni Muumini wake imeshindwa kumuamini na kumuita ili kuwapatia ushauri wa ndani na matokeo yake wanamuacha atoe ushauri huo hadharani jambo ambalo linakuwa sio la afya sana.

kadhalika wengine wamekwenda mbali zaidi na kueleza kwamba hata staili ya Katibu wa NEC Itikadi, Uenezi na Mafunzo wa CCM Paul Makonda imepita mule mule kwa kuangalia nama Mtumishi wa Mungu Mwilisti wa Kimataifa Temba ambavyo amekuwa akitoa mambo makubwa.

"Naye Makonda katika upande wake wa Siasa ametumia njia hiyo hiyo kuzungumza na mwanzoni watu hawakuweza kumuelewa lakini kwa sasa wananchi wengi wameanza kumuelewa na Makonda anaendelea kuzungumza mambo makubwa na kuwa mpatanishi bila kuangalia athari juu ya Jeshi la Polisi, Usalama wa Taifa, Taasisi za Serikali, Mawaziri, Wanasiasa na hata kwenye chama chake hivi karibuni aliweza kuwazodoa Umoja wa Wanaweke Tanzania (UWT) kwa kumnyang'anya mwananchi mmoja nyumba yake na Makonda kuwaamuru wamrejeshee,".

Hivyo wanasema kwamba watu kama kina Makonda wanahitajika katika Taifa la sasa ambapo watu wengi wamekosa haki, kwamba Makonda ameibua mambo mengi na kumfanya DPP kuingilia kati huku akishangaa namna gani umati wa watu umekuwa ukijaa kwenye mikutano ya Makonda ili kusikiliza hekima yake juu ya matatizo ya nchi wakati kuna taasisi zinazohusika na utoaji wa haki hizo lakini hazifuatwi isipokuwa Makonda.

"Lakini hawajiulizi kwa nini watu hawa wanamfuata Makonda na sio Taasisi za Haki, au Ofisi ya DPP imefanya uchunguzi wowote kujua shida inayowakumba wananchi na kukata tamaa katika Taasisi za Serikali za Utendaji haki na kuwakimbilia wanasiasa kama Makonda na kuwasikiliza Watumishi wa Mungu kama Mwinjilisti wa Kimataifa Alphonce Temba ili angalau kupata unafuu wa maisha yao,".

Alipotafutwa kwa njia ya simu Mwinjilisti wa Kimataifa Temba na kuzungumza naye kuhusu mwelekeo wa Makonda wakati huu ambao kumekuwa na sintofahamu ndani ya CCM ikidaiwa kuwa kuna baadhi ya watu hawamuelewi wakidai kwamba amekuja kukivuruga Chama na kueleza kuwa kuna mambo mengine hapaswi kuyafanya na kwamba amepitiliza katika mamlaka ambayo hahusiki,

Katika hilo Mwinjilisti Temba amesema kuwa alilazimika kumtafuta Makonda katika Ulimwengu wa Kiroho, hivyo anasema katika Ulimwengu wa Kiroho ameona Mungu amempa Makonda Mishumaa mitatu kifuani mwake ikiwaka moto.

Mwinjilisti Temba amesema jambo hilo linamaanisha kuwa Makonda anachokifanya anafanya pasipo yeye kujua bali ni kwa msukumo Mkubwa wa Mungu, hivyo ametumia fursa hiyo kuwaonya watu wanaosimama kinyume na Makonda.

Amesema kuwa Makonda wa sasa sio kama yule aliyekuwa Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, na katika kuthibitisha hilo Mwinjilisti Temba anasema kwa sasa Mungu amempatia Makonda karama ya utumishi.
"Anakwenda kuwa Mchungaji pamoja na kazi aliyonayo, Makonda atakuwa Mtumishi wa Mungu, kuna wito ndani yake, itafika mahali umlazimishe huo wito kufanya kazi, pamoja na wito huo wa Mungu atakaokuwa nao, hautamlazimisha aache kazi anayoifanya au aache kuteuliwa au aache kuchapa kazi nyingine, lakini Makonda ni Muhubiri aliyeitwa kufanya kazi za Serikali au za Umma na za kisiasa anazofanya na nyingine nyingi," amesema Mwinjilisti Temba.

Hivyo Mwinjilisti Temba amesema ameona yapo mambo mengi ambayo kama Makonda akihitaji atamwambia yote.

"Mambo ya Mungu ni ya Ajabu sana, kwani Mungu alivyomwita Mtume Paulo kuwa mtumishi Pamoja na kukutana na Maono ya Yesu uso kwa uso lakini cha kushangaza Yesu alimwongoza kukutana na Mtumishi anayeitwa Anania na si wanafunzi wa Yesu wakubwa waliokuwepo kipindi kile hivyo Mungu anampangia mtumishi wa kukusaidia kwa mapenzi yake na uyatii," amesema Mwinjilisti Temba na kuongeza,

"Lakini Mungu amempa huduma, na hii sio mara ya kwanza, niliwahi kumwambia mara ya kwanza wakati tulipokutana katika nyumba ya marehemu Reganarld Mengi alipofariki nyumbani kwake, siku mbili kabla ya kifo cha Mengi nilionyeshwa kwamba mke mdogo wa Mengi atakwenda mahakamani na nilizungumza akiwepo msaidizi wa Mengi nikamueleza kutakwenda kutokea shida ya vurugu kwa sababu mke mdogo atakwenda mahakamani na kutakuwa na mvutano mkubwa juu ya kugombe mali," amebeinisha Mwinjilisti Temba na kusema,

"Na hapo hapo nikaonyeshwa kwamba Makonda atakuwa mtumishi wa Mungu kipindi hicho akiwa Mkuu wa Mkoa hashikiki, haambiliki alikuwa hataki kusikiliza watu, niliongea naye na simu akanikatia, nilimwambia njoo nikupe ujumbe ambao Mungu amenionyesha juu yako Makonda alichelewa sana ndiyo maana alipita mapito makubwa sana akiwa likizo,".

Mwinjilisti Temba anasema kwa wakati huo hakuona sababu ya kumtafuta kwani Makonda mwenyewe hakutaka kuwasiliana naye, na kwamba Mwinjlisti Temba alitaka tu kuwasiliana naye ili kumpatia ujumbe kutoka kwa Mungu na hakuwa akihitaji fedha kutoka kwake.

Hata hivyo Mwinjilisti wa Kimataifa Alphonce Temba ni Mmiliki wa Kampuni ya Kukopesha Fedha (Microfinance) na ni Mmiliki wa Kituo cha Radio Station ambavyo vyote vinafanya kazi vizuri.

Hivyo anasema kwa sasa Mungu amemrudishia ujumbe wa Mkonda, kwamba Makonda anakwenda kuwa Mtumishi wa Mungu ambapo atakuwa Mtumishi wa Injili ambaye pia atakwenda kufanya kazi za Kiserikali, Umma na za Kisiasa kama anazofanya kwa sasa.

"Na hakuna atakayeweza kumpa sumu, wasijisumbue kwasababu ni muitwa, ni mteule wa Bwana. Mengine yote ya Makonda nawaambia Watanzania wayasahau, kwanini Watanzania wengi wanavutwa na Makonda, sio kwa sababu anaongea vizuri, sio kwasababu Makonda anazungumza hizi shida, mambo haya anayozungumza Makonda yanazungumzwa na watu wengi kwenye vikao vya vijiji na yanazungumzwa na watu wengi kwenye mitandao, yanazungumzwa na wanasiasa na viongozi wa vyama vya upinzani akina Zitto, Lissu, Mbowe na watumishi wote wanazungumza, wananchi wanalalamika lakini hazikupata mvuto wa uitikio, wala kuwatoa machozi,".

Hivyo Mwinjilisti Temba anasema kuwa tofauti iliyopo kwa Makonda ni kuitwa kwake katika utumishi wa Mungu na Msukumo wa Kimungu, kwamba katokana na hali hiyo wapo watu watakao kwenda kusimama mbele ya Makonda ambao wataanguka na kuzimia wakati akisema shida zao.

Kwamba pamoja na kuanguka hakuna atakayekufa kwani watapepewa na kuamka, Mwinjilisti Temba anasema hiyo ni ishara ambayo inadhihirisha namna alivyomuuona mwanzo na mwisho wake, na kusisitiza kuwa anachokiona kwa sasa kwa Makonda ni mishumaa mitatu kifuani mwake inayowaka moto.

"Na kazi anayoifanya ni kazi ya upinzani ndani ya chama chake, amewakilisha sauti ya upinzani, labda nimshauri kitu kimoja kwa sababu wakati mwingine na yeye hajui anachokifanya, hivyo hana sababu ya kuwagusa kwa sasa wapinzani, hana sababu ya kuzungumzia tena Chadema, hana sababu ya kuzungumzia tena ACT, wala CUF, wala ADC, Makonda zungumzia shida za wananchi, zungumzia sera za chama, zungumzia uwajibikaji ndani ya taasisi, uwajibikaji wa viongozi, usimuogope kiongozi yeyote, waheshimu viongozi walioko juu waliokupa nafasi hiyo, endelea kuwa mnyenyekevu kwao na kwa Watanzania, utauona mkono wa Mungu juu yako," amesema Mwinjilisti Temba.

Aidha Mwinjilisti Temba amewakumbushia Watanzania juu ya Unabii wake wa mwishoni mwa maka jana alioutoa na kusema umeanza kutimia na bado mengi yanakuja cha kufanya ni kufuata maelekezo aliyoyatoa hivyo wale ambao hawajausoma wautafute au wawasiliane naye. (Mawasilano ni +255755973787).

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news