Matumizi ya Mfumo wa Usaili wa Kidigitali unakuza uwazi kwenye mchakato wa kutoa ajira serikalini-Naibu Waziri Kikwete

NA LUSUNGU HELELA

NAIBU Waziri Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete amesema kitendo cha Sekretarieti ya Ajira katika Utumishi wa Umma kuanza kutumia rasmi mfumo wa usaili wa kidigitali unaomuwezesha mwombaji kusailiwa eneo alilopo badala ya kusafiri umbali mrefu, ili kupunguza gharama kwa Serikali na kwa wanaosailiwa ni mafanikio makubwa ya Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Uongozi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan katika kukuza uwazi kwenye mchakato wa kutoa ajira.
Mhe. Kikwete ametoa kauli hiyo jajanjijini Dar es Salaam mara baada ya kushuhudia wasailiwa wa kada ya Tehama wakifanya usaili huo katika Chuo Kikuu cha St. Joseph , ikiwa ni moja ya kituo cha usaili wa mchujo unaofanyika kidigitali katika kila Mkoa Nchi nzima, ikiwa ni usaili wa kwanza tangu mfumo huo ulipozinduliwa hivi karibuni.

Amesema, mfumo huo umeanza kutumika wakati sahihi ambapo Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan anaendelea na jitihada za kuimarisha uwazi na kuepuka upendeleo katika suala zima la utoaji ajira serikalini.
Amesema,vituo vipatavyo 32 nchi nzima leo vimeendesha usaili huo ambapo jumla ya wasailiwa 2325 wamepata fursa ya kufanya usaili huo pasipo kulazimika kusafiri umbali mrefu

Amefafanua kuwa, vituo 32 kulikofanyika usaili huo kunajumuisha Tanzania Bara na Visiwani ambapo kwa Mkoa wa Dar es Salaam kulikuwa na vituo vinne kutokana na idadi kubwa ya wasailiwa waliokuwa wameomba

Mhe.Kikwete amesema, suala la ajira ni maisha ya watu, hivyo mchakato huo leo umefungua ukurasa mpya wa kukuza uwazi na uadilifu katika kuondoa manung'uniko kwa wale ambao wanatafuta ajira serikalini.
Amesema, mfumo huo mbali ya kusaidia kupunguza gharama za wasailiwa ambao walikuwa wanalalamika kusafiri umbali mrefu kwenda kwenye kituo cha usaili kwa kutumia muda mwingi na gharama kubwa, ila leo hii wamesailiwa mahali walipo na kisha kuendelea kufanya shughuli zingine za kujiingizia kipato.

Kwa upande wake Mkuu wa Idara ya Tehama kutoka Sekretarieti ya Ajira katika Utumishi wa Umma, Mhandisi Samweli Tanguye amesema mfumo huo mara baada ya wasailiwa hao kumaliza kufanya mchujo watapata matokeo yao leo tofauti na ilivyokuwa mwanzo ambapo matokeo hayo yalikuwa yakichukua zaidi ya siku tatu kutoka.

Amesema, mfumo huu unatoa nafasi kwa Wasailiwa ambao wanafanya usaili zaidi ya mmoja ndani ya siku moja kuwa wigo wa kufanya usaili mwingine siku hiyo hiyo kwa saa tofauti ambapo awali haikuwa rahisi.
Kwa upande wake Juma Ali, Msailiwa wa kada ya Tehama amepongeza ujio wa mfumo huo wa usaili wa kidijitali huku akisema licha ya kumpunguzia gharama ya kusafiri hadi Jijini Dodoma lakini amepata fursa ya kuendelea kufanya shughuli zingine mara baada ya kumaliza usaili wake.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news