BENKI Kuu ya Tanzania, kama wakala wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inapenda kuutaarifu umma na wawekezaji kwamba imebadili kiwango cha juu cha ushiriki katika dirisha lisilo la ushindani kutoka kiasi cha TSH 50,000,000 hadi TSH 500,000,000 kwa kila mnada.
Mabadiliko haya yanalenga kuongeza ushiriki wa wawekezaji na kuboresha ufanisi wa upangaji bei katika minada ya dhamana za Serikali.
Wawekezaji wanaotaka kutumia dirisha lisilo la ushindani wanakumbushwa kuwa utaratibu wa uwasilishaji wa zabuni na mgawanyo wa kiasi kilichopangwa katika dirisha hilo hautabadilika.
Hivyo basi, wawekezaji wanapaswa kuendelea kuwasilisha zabuni zao kwa Benki Kuu ya Tanzania kupitia kwa mawakala wa uwekezaji, wakionyesha tarehe ya mnada, namba ya mnada, muda wa kuiva na kiasi cha uwekezaji.
Aidha, zabuni zisizo za ushindani zitaendelea kugawiwa kwa kutumia bei ya wastani iliyopatikana kutoka katika zabuni za ushindani za mnada husika.
Kwa maelezo zaidi au ufafanuzi, tafadhali wasiliana na wakala wako wa uwekezaji katika dhamana za serikali au Benki Kuu ya Tanzania kupitia Kurugenzi ya Masoko ya Fedha (kwa barua pepe; info@bot.go.tz).