Benki zatakiwa kuimarisha usimamizi wa vihatarishi vya mikopo na kudumisha uadilifu

DAR-Wadau wa sekta ya fedha nchini wametakiwa kuimarisha mbinu zao za usimamizi wa vihatarishi vya mikopo na kuhakikisha uadilifu katika utekelezaji wa shughuli zao za kila siku ili kulinda uthabiti wa mfumo wa fedha na kusaidia utoaji wa mikopo kwa njia salama na endelevu katika taasisi zao.
Wito huo umetolewa na Mkurugenzi wa Usimamizi wa Sekta ya Fedha, Benki Kuu ya Tanzania (BoT),Bw. Sadati Musa wakati wa ufunguzi rasmi wa warsha kuhusu usimamizi wa vihatarishi vya mikopo kwa maofisa wa mikopo kutoka mabenki na taasisi mbalimbali za kifedha.
Bw. Sadati amepongeza juhudi za sekta hiyo katika kuboresha usimamizi wa hatari za mikopo, na kueleza kuwa kiwango cha mikopo chechefu (NPLs) kimeshuka kutoka asilimia 9.42 mwaka 2020 hadi asilimia 3.43 kufikia Mei 2025.

Hata hivyo, amesisitiza kuwa bado kuna kazi ya ziada inayopaswa kufanywa na kila benki katika kuboresha mifumo yao ya udhibiti wa ndani na usimamizi wa vihatarishi.
Bw. Sadati ameelezea umuhimu wa kuwajengea wafanyakazi wa benki uwezo na kuwapa nyenzo sahihi za kupunguza hatari hizo kwa ufanisi huku akiwataka washiriki kutumia fursa hiyo kushiriki kikamilifu katika mijadala na kubadilishana uzoefu kwa vitendo ili kuimarisha uwezo wa pamoja wa sekta.

Warsha hiyo inayofanyika katika Ofisi za Makao Makuu Ndogo ya Benki Kuu ya Tanzania jijini Dar es Salaam kuanzia tarehe 16 hadi 20 Juni 2025, inatarajiwa kujadili masuala mbalimbali yanayohusu usimamizi wa vihatarishi vya mikopo.
Vilevile masharti ya kisheria, usimamizi wa mali zenye hatari, kushughulikia mikopo chechefu, upangaji madaraja ya mikopo na uwekaji wa akiba, pamoja na matumizi ya mabaraza ya kumbukumbu za wakopaji.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

Know matter how large or small your business is, advertising here