SINGIDA-Waziri wa Fedha, Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba, ameshiriki Harambee Kuu ya Kanisa la Kiinjili la Kilutheri (KKKT) Dayosisi ya Kati na kufanikisha kukusanya fedha zaidi ya shilingi bilioni moja zitakazotumika kujenga Hospitali.
Harambee hiyo iliyofanyika leo tarehe 29 Juni, 2025 akiwa Mgeni Rasmi katika Ibada iliyoongozwa na Mkuu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Askofu Dkt. Alex Gehaz Malasusa,) kwa kushirikisha na waumini mbalimbali kutoka ndani na nje ya Dayosisi hiyo.
Mhe. Dkt. Nchemba amewashukuru waumini wote walioshiriki katika harambee hiyo muhimu kwa dayosisi na kuwasihi kuendelea kumtumaini Mungu kupitia matoleo yao katika kufanikisha shughuli za Kijamii kusonga mbele huku akiwasihi Waumini wa dhehebu hilo na madhehebu mengine nchini kuendelea kudumisha amani na mshikamano uliopo katika Taifa linapoelekea Uchaguzi Mkuu Oktoba 2025.
Kwa upande wake Mkuu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Askofu Dkt. Alex Gehaz Malasusa, wakati wa muhubiri yake amesema Imani waliyonayo Watanzania kwa Serikali yao katika kulinda umoja, upendo na mshikamano uliopo ni kubwa hivyo Taifa liendeleze mshikamano huo kwa nguvu zote.
Ameongeza kuwa, Kanisa lina mchango mkubwa katika kudumisha amani na kujenga nyumba za Ibada zinazotumika kutoa huduma muhimu kwa Wananchi ikiwemo Vituo vya kulelea Watoto, Hospitali na kuwalea kiroho waumini wake wakati wote.
Pia amemshukuru Mhe. Dkt. Nchemba kwa kujitolea katika shughuli mbalimbali za Kidini zinazofanyika na kuhakikisha huduma hiyo inaboreshwa katika maeneo mbalimbali hapa nchini.










