RUVUMA-Katika bonde la kijani lililojaa mandhari ya kuvutia Kusini mwa Tanzania, Wilaya ya Namtumbo mkoani Ruvuma sasa inang’aa kama nyota mpya ya utalii.
Kupitia uwekezaji wa shilingi bilioni 2.1 kutoka Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, fedha hizo zimetumika kujenga miundombinu ya Hifadhi ya Taifa ya Nyerere ikiwemo lango la kisasa la kuingia Hifadhi ya Taifa ya Nyerereambalo limejengwa eneo la Likuyuseka Maganga na sasa, ndio mlango rasmi wa watalii kuingia hifadhi hiyo kupitia Nyanda za Juu Kusini.
Akizungumza kwa furaha hivi karibuni, Mkuu wa Wilaya ya Namtumbo, Mhe. Ngollo Malenya, anasema ujenzi wa lango hilo umekamilika na sasa wilaya yake ipo tayari kuwakaribisha wageni kutoka kila pembe ya ukanda wa kusini,ikiwemo mikoa ya Lindi, Mtwara, Njombe, Iringa, Mbeya hadi Ruvuma, na hata nchi jirani kama Msumbiji na Malawi.
“Lango hili ni fursa ya kipekee kwa Namtumbo na Mkoa wa Ruvuma. Linakuza uchumi wetu kwa haraka na linafungua njia ya uwekezaji mkubwa kwenye sekta ya utalii,” anasisitiza Malenya huku akitoa rai kwa wawekezaji wa ndani na nje kuwekeza kwenye ujenzi wa hoteli, huduma za utalii na miundombinu mingine muhimu.
Tags
Habari
Hifadhi ya Taifa ya Mwalimu Julius Nyerere
Sekta ya Utalii Tanzania
Wizara ya Maliasili na Utalii Tanzania


