Sera ya Madini yawafikia wanafunzi Dodoma

DODOMA-Wizara ya Madini imeendelea kutoa elimu kwa umma kuhusu mnyororo wa thamani wa madini, safari hii ikiwa ni kwa wanafunzi kutoka shule mbalimbali za Msingi na Sekondari waliotembelea banda la wizara hiyo katika maonesho ya Wakulima Nanenane yanayoendelea jijini Dodoma.
Akizungumza katika banda la Wizara hiyo Mhandisi Jovina Prosper kutoka Wizara ya Madini amesema kuwa wizara hiyo imekuwa mstari wa mbele katika kutoa elimu kuhusu sekta ya madini kwa makundi mbalimbali, yakiwemo makundi ya wanafunzi ili kuwajengea uelewa wa kina juu ya mchango wa sekta ya madini katika maendeleo ya taifa.
“Tumekuwa tukitoa elimu kuhusu mnyororo wa thamani wa madini kuanzia hatua ya utafiti, uchimbaji, uchenjuaji na masoko. Lengo letu ni kuhakikisha kuwa wanafunzi hawa wanapata uelewa wa kina kuhusu jinsi sekta hii ilivyo muhimu kwa maendeleo ya nchi yetu,” amesema Mhandisi Jovina.

Aidha, amefafanua kuwa Wizara ya Madini inasimamia utekelezaji wa Sera ya Madini ya Mwaka 2009, ambayo imekuwa mwongozo muhimu katika kuhakikisha kuwa shughuli za uchimbaji na biashara ya madini zinakuwa na tija kwa taifa na zinawanufaisha Watanzania kwa ujumla.

“Wizara inatekeleza Sera hii kwa kuhakikisha rasilimali za madini zinachangia kikamilifu katika pato la taifa, huku tukilinda mazingira na kuhakikisha ushirikishwaji wa Watanzania katika shughuli zote za madini,”ameongeza Mhandisi Jovina.

Wanafunzi walionufaika na elimu hiyo wameonesha kufurahishwa na fursa ya kujifunza kwa vitendo, huku wakieleza kuwa elimu waliyopata imewasaidia kuelewa zaidi kuhusu umuhimu wa sekta ya madini na jinsi wanavyoweza kushiriki katika shughuli za kimaendeleo kupitia sekta hiyo.
Maonesho hayo yamekuwa jukwaa muhimu kwa taasisi mbalimbali za serikali kutoa elimu kwa umma na kuhamasisha ushiriki wa wananchi, hususan vijana, katika sekta za kimkakati kama vile madini, kilimo, nishati na teknolojia.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news