DAR-Wajumbe wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) wamefanya maamuzi magumu kupitia kura za maoni katika uchaguzi wa kuchagua wagombea udiwani na ubunge ambao watakiwakilisha chama hicho Uchaguzi Mkuu utakaofanyika Oktoba 29,2025.


Katika kura za maoni zilizofanyika Agosti 4, 2025 katika maeneo mbalimbali nchini, baadhi ya waliokuwa wanatetea nafasi zao za ubunge wameachwa kwa kura nyingi, huku kura za maoni zikileta sura mpya.
Jimbo la Muleba Kaskazini, Adonis Bitegeko ameibuka mshindi kwenye kura za maoni za CCM kwa kumbwaga aliyewahi kuwa Waziri wa Viwanda na Mbunge wa muda mrefu, Dkt. Charles Mwijage.
Katika Jimbo la Vunjo,Dkt.Charles Kimei ambaye amekuwa mbunge tangu 2020 ameangushwa na Enock Zadock Koola aliyeibuka mshindi kwa kura 1,999 dhidi ya Kimei aliyepata kura 861.
Aidha,Moshi Vijijini, Profesa Patrick Ndakidemi amepoteza mbele ya Moris Makoi, aliyekuwa Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Moshi. Makoi alipata kura 2,148 huku Ndakidemi akijikusanyia kura 627 pekee.
Jimbo la Iringa Mjini aliyekuwa mbunge Jesca Msambatavangu amejikuta nafasi ya nne kwa kura 408. Mshindi wa kura hizo ni Fadhil Ngajilo aliyepata kura 1,899, akifuatiwa na Wakili Moses (1,523) na Mchungaji Peter Msigwa (477).
Kyerwa, Mbunge Innocent Bilakwate ameangushwa na Khalid Nsekela aliyezoa kura 5,693 sawa na asilimia 71 huku Bilakwate akipata kura 1,567.
Katika Jimbom la Makambako, Katibu Mkuu wa zamani wa CCM, Daniel Chongolo ameibuka mshindi wa kishindo kwa kura 6,151, na kumwacha mbali Deo Sanga (maarufu kama Jah People), aliyekuwa mbunge wa jimbo hilo kwa miaka 15, ambaye alipata kura 470 tu sawa na asilimia 7.1.
Mtwara Mjini, Joel Arthur Nanauka ameibuka mshindi kwa kura 2,045 dhidi ya Hassan Mtenga Mbunge anayemaliza muda wake aliyepata kura 1,607.
Tabora Mjini, Shabani Mrutu ameongoza kwa kura 6,612, akimshinda kwa mbali aliyekuwa mbunge Emmanuel Mwakasaka aliyepata kura 228 pekee. Mwakasaka alizidiwa hata na wapinzani wengine kama Hawa Mwaifunga (326) na Kisamba Tambwe (395).
Geita Mjini, Constantine Kanyasu ambaye amehudumu kwa miaka 10, amepata kura 2,097 na kushindwa na Chacha Wambura aliyepata kura 2,145. Upendo Peneza alipata kura 1,272.
Katika jimbo la Namtumbo, aliyekuwa Mbunge Vita Kawawa ameshindwa mbele ya Dkt.Juma Zuberi Homera, aliyekuwa Mkuu wa Mkoa wa Mbeya. Homera alipata kura 11,836 asilimia 92 huku Kawawa akipata kura 852.
Jimbo jipya la Katoro, aliyekuwa Mbunge wa Busanda, Tumaini Magesa, alihamia huko lakini akashika nafasi ya tatu kwa kura 1,265 nyuma ya Kija Ntemi (2,134) na Ester James (2,075).
Vilevile Jimbo la Lindi Mjini, Mbunge anayemaliza muda wake, Hamida Abdalla, ameangushwa na Mohamed Utali, aliyeibuka kidedea kwa kupata kura 1,474 kati ya kura 3,289 zilizopigwa.
Hamida alipata kura 876 pekee, ishara ya wazi kuwa wajumbe wameamua kubadili mwelekeo wa uongozi katika eneo hilo.
Nyasa, aliyekuwa Mbunge na Naibu Waziri wa zamani, Stella Manyanya, ameangushwa kwa kishindo na John Nchimbi, aliyepata kura 9,157 kati ya kura 10,695 zilizopigwa.
Manyanya alipata kura 548 tu, matokeo ambayo ni pigo kubwa kwa mbunge huyo mkongwe aliyedumu kwa vipindi kadhaa ndani ya Bunge.
Pia,Katibu wa Hamasa na Chipukizi UVCCM Mkoa wa Katavi, Laurent Luswetula ameongoza kura za maoni CCM Jimbo la Kavuu.
Laurent mwenye shahada ya uzamili ya uhasibu na fedha ameongoza kwa kura 1564, akifuatiwa na Pudensia Kikwembe aliyepata kura 1065, huku mbunge aliyemaliza muda wake Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Geoffrey Pinda akishika nafasi ya tatu kwa kupata kura 1,032.
ORODHA YA WABUNGE WALIOONGOZA KURA ZA MAONI CCM