ARUSHA-Wanafunzi wa Shule ya Sekondari Tumaini Senior wilayani Karatu, mkoani Arusha, wamebuni teknolojia ya ulipaji wa huduma ya maji kupitia simu kabla ya matumizi, ili kurahisisha huduma kwa wateja na kupunguza muda mrefu wa malipo ya ankara za maji.
Ubunifu huo umeoneshwa na wanafunzi wa kidato cha tatu katika maonesho ya teknolojia shuleni hapo, wakiongozwa na mwanafunzi kinara, Lepapa Alaisi, ambaye alisema masomo ya ziada ya sayansi na ubunifu pamoja na fursa ya kusoma sayansi ya kompyuta tangu kidato cha kwanza ndiyo yaliyochochea ubunifu huo.Mmoja wa wazazi waliokuwepo, Eliakim Akyoo, amepongeza ubunifu wa wanafunzi hao na kuhamasisha uongozi wa shule kuendeleza masomo ya sayansi na ubunifu, pamoja na kuwalea kikamilifu wanafunzi wabunifu wenye vipaji mbalimbali.
Aidha, Mkurugenzi wa shule za Tumaini Senior na Tumaini Junior, Modest Bayo, amesema kuwa kuanzisha masomo ya sayansi ya kompyuta tangu kidato cha kwanza kumechochea upatikanaji wa ajira kwa wahitimu kutokana na umahiri wa utengenezaji mifumo."Watoto wa Tumaini Senior wakianza kidato cha kwanza wanaanza na somo la sayansi ya kompyuta, ambalo sasa litafundishwa kama mtaala mpya, na limewasaidia kupata ajira hata wakiwa fresh form four, na wapo wanne waliwahi kufanya kazi na kampuni ya programu tumizi ya Google," amesema Bayo.