TAEC yatoa Elimu ya Mionzi kwa wanafunzi 9,391 wa sekondari mkoani Tanga

TANGA-Katika dunia inayozidi kutegemea teknolojia, elimu sahihi kuhusu matumizi salama ya mionzi na teknolojia ya nyuklia imekuwa nguzo muhimu ya maendeleo.
Tume ya Nguvu za Atomu Tanzania (TAEC) imechukua jukumu hilo kwa uzito mkubwa, kwa kuendesha kampeni ya elimu ya mionzi kwa wanafunzi wa shule za sekondari mkoani Tanga,hatua inayolenga kuvunja mitazamo potofu na kuhamasisha kizazi kipya kuelekea sayansi.

Elimu ya Mionzi ni Maisha

Kwa muda mrefu, teknolojia ya nyuklia imekuwa ikihusishwa na hofu ya silaha za maangamizi.Lakini ukweli ni kwamba, teknolojia hii ina mchango mkubwa katika sekta za afya, kilimo, viwanda na mazingira.
TAEC imeamua kuondoa hofu hiyo kwa kuwafikia wanafunzi 9,391 kutoka shule 10 za sekondari zikiwemo Chumbageni, Galanosi, Kiomoni, Mikanjuni, Mkwakwani, Usagara, Nguvumali, Pongwe, Mabokweni, na Msambweni ndani ya wiki moja tu, kuanzia tarehe 22 hadi 26 Septemba 2025.

Kupitia mafunzo ya vitendo, mijadala ya papo kwa papo, na maonesho ya vifaa vya mionzi, wanafunzi walipata fursa ya kujifunza matumizi salama ya teknolojia ya nyuklia na faida zake katika maisha ya kila siku.

Uhimu wa kampeni

Wanafunzi walijifunza kuwa mionzi si hatari kila inapopatikana. Teknolojia ya nyuklia hutumika kuchunguza na kutibu magonjwa kama saratani, kuboresha mbegu za kilimo, kusafisha maji, na kuongeza ubora wa bidhaa viwandani. Elimu hii inasaidia jamii kutegemea maarifa badala ya uvumi.

TAEC inalenga kuwahamasisha wanafunzi kuchukua masomo ya Fizikia, Kemia, Baiolojia na Hisabati masomo yanayohitajika kwa taaluma kama fizikia tiba, usalama wa mionzi, na uhandisi wa nyuklia. Hii ni uwekezaji wa moja kwa moja katika rasilimali watu ya taifa.
Pia,Radiotherapy ni mojawapo ya tiba bora ya saratani inayotegemea teknolojia ya mionzi.

Kupitia kampeni hii, wanafunzi walielewa jinsi teknolojia ya nyuklia inavyoweza kuokoa maisha, na umuhimu wa kuwa na wataalamu waliobobea katika sekta hiyo.

Kulinda Usalama wa Jamii na Mazingira

Matumizi yasiyodhibitiwa ya mionzi yanaweza kuwa hatari. Kwa kuwapa elimu mapema, vijana wanajengewa uwezo wa kuchukua tahadhari na kuelewa taratibu za usalama wa mionzi, jambo muhimu kwa usalama wa jamii na mazingira.

Vilevile,kampeni hii inachangia moja kwa moja katika SDG 3 (Afya Bora), SDG 4 (Elimu Bora), SDG 7 & 9 (Nishati na Viwanda), na SDG 13 (Ulinzi wa Mazingira). Elimu ya mionzi ni nyenzo ya kufikia maendeleo ya kweli na endelevu.

Sayansi si ya wenye akili pekee

Moja ya changamoto kubwa kwa wanafunzi ni mtazamo kwamba masomo ya sayansi ni magumu au ni ya watu maalum tu.

TAEC imebadili hali hiyo kwa kutumia mbinu shirikishi, zinazowahusisha wanafunzi moja kwa moja. Kwa njia hii, wanafunzi wanajenga ujasiri na shauku ya kuchunguza zaidi, huku walimu wakiboresha mbinu za kufundisha kwa njia ya kuvutia.
Aidha,kampeni ya TAEC si ya muda mfupi, bali ni sehemu ya mkakati wa muda mrefu wa kuandaa taifa lenye maarifa ya sayansi ya nyuklia kwa maendeleo endelevu.

Kwa kuwafikia wanafunzi zaidi ya 9,000 ndani ya wiki moja, TAEC imedhihirisha dhamira ya dhati ya kuandaa kizazi kitakacholinda maisha, mazingira, na kuchochea maendeleo ya viwanda vya kisasa.
"Wanafunzi hawa si wasikilizaji tu, bali ni wataalamu wa kesho. Elimu wanayoipata leo, ndiyo itakayoweka msingi wa taifa lenye afya, ulinzi wa mazingira na maendeleo ya viwanda.”

Kwa taarifa zaidi kuhusu kampeni za elimu ya mionzi mashuleni, tembelea tovuti rasmi ya TAEC au wasiliana na ofisi zao za kanda.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news