KAGERA-Mahakama ya Hakimu Mkazi Bukoba, mkoani Kagera imemtia hatiani mkulima, Bw. Anthony Mutagwaba Kagombora kwa tuhuma za rushwa.
Hukumu hiyo ya shauri la rushwa namba 24775/2025 imetolewa Oktoba 10,2025 na Hakimu Mkazi Mfawidhi,Mheshimiwa Janeth Massesa.Shauri hilo liliendeshwa na Mwendesha Mashtaka wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) Mkoa wa Kagera, Daudi Jacob Oringa.
Chini ya kifungu cha 15 cha Sheria ya Kuzuia Rushwa Sura ya 329 Marejeo ya 2023,mkulima huyo ilidaiwa kwa njia ya rushwa alijipatia kiasi cha shilingi 1,626,570 kutoka Chama cha Ushirika KIHUMULO AMCOS ikiwa ni malipo ya kahawa aina ya Robusta.
Ni msimu wa mwaka 2024/2025, huku akijua yeye sio mwanachama na hakuuza kahawa katika chama hicho kwa kipindi cha mwaka 2024/2025.
Aidha,baada ya Mshtakiwa kutiwa hatiani ametakiwa kulipa faini ya shilingi 500,000 au kwenda jela mwaka mmoja na kutakiwa kurejesha kiasi cha shilingi 1,626,570 kwenye Chama cha Ushirika KIHUMULO AMCOS ndani ya miezi mitatu.Mshtakiwa amelipa faini.
Tags
Habari
Mahakamani Leo
PCCB Tanzania
Robusta Coffee
Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU)