Serikali yapandisha mishahara sekta binafsi

DAR-Serikali ya Awamu ya Sita imefanikiwa kutangaza nyongeza ya Kima cha chini cha Mshahara kwa sekta binafsi kwa wastani wa asilimia 33.4 kutoka Shilingi 275,060 hadi 358,322 ambapo kitaanza kutumika rasmi ifikapo Januari 1, 2026 hatua inayolenga kuongeza tija ya uzalishaji na kuinua maslahi ya wafanyakazi nchini.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu- Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu Ridhiwani Kikwete akitangaza kwa umma amri ya kuhusu kupandishwa kwa kima cha chini cha mshahara kwa sekta binafsi nchini Oktoba 17,2025 jijini Dar es Salaam.

Akitangaza amri hiyo Oktoba 17,2025 jijini Dar es Salaam wakati akizungumza na waandishi wa habari Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu -Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu Ridhiwan Kikwete alisema mchakato wa upangaji wa Kima kipya cha chini cha mshahara umekamilika na kwamba umezingatia mamlaka aliyopewa chini ya Kifungu cha 39 (1) cha Sheria ya Taasisi za Kazi, Sura 300.

“Kwa mujibu wa Amri hiyo, Sekta za Kima cha chini cha Mshahara zimeongezeka kutoka 13 za mwaka 2022 hadi 16 kwa mwaka 2025 na kutoka sekta ndogo 25 za mwaka 2022 hadi 46 kwa mwaka 2025. Kima cha chini cha mshahara kimeongezeka kwa wastani wa asilimia 33.4 kutoka shilingi 275,060 hadi 358,322 na kitaanza kutumika rasmi tarehe 1 Januari, 2026,” alisema Waziri Ridhiwani Kikwete.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu- Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu Ridhiwani Kikwete akitangaza kwa umma amri ya kuhusu kupandishwa kwa kima cha chini cha mshahara kwa sekta binafsi nchini Oktoba 17,2025 jijini Dar es Salaam.

Kwa mujibu wa Waziri Ridhiwani , Amri ya Kima cha Chini cha Mshahara imegusa sekta za kilimo, afya, mawasiliano, usafirishaji, hoteli, madini, biashara na viwanda, shule binafsi, huduma za ulinzi binafsi, nishati, uvuvi na huduma ya baharini, michezo na utamaduni pamoja na huduma nyinginezo.
Mwenyekiti wa Bodi ya Kima cha Chini cha Mishahara kwa Sekta Binafsi Dkt. Suleiman Rashid Mohamed akizungumza Oktoba 17,2025 kuhusu namna sekta binafsi ilivyoshiriki kwenye mchakato wa majadiliano kuhusu kupanda kwa kima cha chini cha mshahara kwa wafanyakazi sekta binafsi ambapo ambapo ameeleza kuridhishwa na mchakato huo.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Bodi ya Kima cha Chini cha Mishahara kwa Sekta Binafsi,Dkt. Suleiman Rashid Mohamed alisema mchakato wa majadiliano ulikuwa shirikishi ambapo vyama vya wafanyakazi, waajili na waajiliwa vilishiriki kikamilifu katika hatua zote.
Naibu Katibu Mkuu Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi Tanzania (TUCTA), Rehema Ludanga akieleza faraja walionayo wafanyakazi wa sekata binafsi baada ya amri ya serikali kuhusu kupandishwa kima cha chini cha mshahara kulikotangazwa leo na serikali jijini Dar es Salaam.

Naye Naibu Katibu Mkuu Shirikishio la Vyama vya Wafanyakazi Tanzania (TUCTA),Rehema Ludanga alisema kitendo cha Serikali kutangaza amri ya kupanda kwa mishahara kwa kima cha chini cha sekta binafsi ni faraja kwa wafanyakazi nchini kwani kimeonesha dhahili namna Serikali inavyothamini maslahi ya wafanyakazi nchini.

Rehema aliongeza kusema ni wakati sasa waajili wote katika sekta binafsi kutekeleza amri hiyo kwa kupandisha mishahara ikibidi zaidi ya kiwango kilichotangazwa ili kuongeza maslahi bora ya wafanyakazi wao.
Afisa Mtendaji Mkuu wa Chama cha Waajili Tanzania (ATE),Suzzane Ndomba- Doran amewataka waajili nchini kujipanga kufanya utekelezaji wa amri juu ya kuongeza mishahara kwa watumishi wa sekta ya umma kwa kuwa chama kilishiriki mchakato huo kupitia maoni yaliyokusanywa kwenye mikoa yote nchini.

Suzanne Ndomba-Doran ambaye ni Afisa Mtendaji Mkuu Chama cha Waajili Tanzania (ATE) akizungumza kwenye kikao hicho alisema,Chama kilishiriki kikamilifu kwenye mchakato kupitia kamati ya wataalam ambapo maoni yote yaliyokusanywa toka mikoa yote nchini na yamefanyiwa kazi hatua inayotoa urahisi wa utekelezaji wa amri hiyo..

Aidha, Mtendaji Mkuu huyo aliwasihi waajili kutumia muda huu kabla ya kufika tarehe 01 Januari 2026 kufanya mazungumzo yatakayopelekea kubadilisha ulipaji wa mishahara kwa mujibu wa amri iliyotangazwa na Serikali na kwamba ATE itaendelea kutoa elimu na taarifa kwa waajili wote nchini kutekeleza amri hii.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news