TABORA-Jeshi la Polisi likishirikiana na Serikali katika Wilaya ya Kaliua mkoani Tabora limeendesha Mashindano ya Mpira wa Miguu baina ya timu ya polisi wilayani humo na maafisa usafirishaji maarufu kama bodaboda lengo ikiwa ni kuendelea kukomaza Mahusiano ya Jeshi la Polisi na wananchi.
Katika mashindano hayo ambayo yamefanyika Disemba 13,2025 katika Uwanja wa Kolimba Mjini Kaliua awali akizungumza Kamanda wa Jeshi la Polisi Mkoa wa Tabora Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Jeshi la Polisi (Sacp) Richard Abwao amewataka Wananchi hasa vijana kuwa mabalozi wa kulinda amani na sio kutumika katika vitendo vinavyochochea uvunjifu wa amani.
Mkuu wa Wilaya ya Urambo,Mhe. Dkt.Khamis Mkanachi akimwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Tabora Bwana Paul Chacha katika Mashindano hayo mbali na kutoka pongezi kwa Jeshi la Polisi kwa hatua ya kuendelea kujenga Mahusiano imara na Wananchi amesema kuwepo kwa utulivu ni sababu tosha ya kuwafanya kujiimarisha kiuchumi kupitia shughuli zao za kila siku.
Kwa upande wao baadhi ya Wananchi wakiwemo Maafisa usafirishaji (Bodaboda) John Venas na Mihayo Peter wameishukuru Serikali ya Wilaya hiyo kwa kushirikiana na Jeshi la Polisi katika kuandaa Mashindano hayo huku wakieleza kuendelea kutoka ushirikiano wa dhati kwa Jeshi la Polisi katika kukabiliana na vitendo vya uhalifu na uvunjifu wa amani.











