DODOMA-Jeshi la Polisi nchini Tanzania kwa kushirikiana na vyombo vingine vya ulinzi na usalama nchini wamewahakikishia wananchi kuwa wataendelea kulinda usalama wa Tanzania sambamba na maisha na mali za wananchi ili waweze kuendelea na shughuli zao kwa amani, utulivu na usalama.
Hayo ni kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Msemaji wa Jeshi la Polisi Makao Makuu, Naibu Kamishna wa Polisi,DCP David Misime leo Disemba 10, 2025.
Kupitia taarifa hiyo,Jeshi la Polisi limeonya pia kuhusu wanaopanga kujitokeza leo kwenye mitaa mbalimbali ili kufanya kile kinachoitwa maandamano ya amani baada ya kushindwa kuyafanya jana Desemba 9, 2025.
"Jeshi la Polisi linaendelea kuwakumbusha, kuwasisitiza na kuwaonya wasifanye hivyo kwani wanachokiita maandamano ya amani yasiyo na kikomo yalipigwa marufuku kutokana na kukosa sifa kulingana na matakwa ya Katiba na sheria ya Polisi na Polisi wasaidizi sura 322," amesema Misime.
Polisi pia imeeleza kuwa,kwa ambaye atakaidi kutii sheria za nchi kwa lengo la kuhatarisha usalama wa nchi ili kusimamisha shughuli za kiuchumi na kijamii zisiendelee, watadhibitiwa ili nchi ibaki salama na watanzania wema na wapenda amani wabaki salama.
Vilevile,taarifa ya polisi imetoa wito kwa wananchi kuendelea kufanya shughuli zao na kufuata maelekezo watakayokuwa wanapewa na vyombo vya ulinzi na usalama katika maeneo yote nchini.
Sambamba na kutii sheria za nchi ili taifa liendelee kuwa salama na kila mmoja kuweza kuendelea na shughuli zake.
