ZANZIBAR-Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mheshimiwa Dkt. Hussein Ali Mwinyi ameunda Tume Maalum ya Kupitia na Kutathmini Masuala ya Fidia yanayotokana na utekelezaji wa miradi mbalimbali ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika maeneo tofauti ya Unguja na Pemba.
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi,Mheshimiwa Dkt.Hussein Ali Mwinyi.
Uamuzi huo umechukuliwa kufuatia changamoto zilizojitokeza katika utekelezaji wa masuala ya fidia, hali ambayo imekuwa ikisababisha malalamiko kutoka kwa wananchi na kuathiri kasi ya utekelezaji wa baadhi ya miradi ya maendeleo.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Ofisi ya Rais, Ikulu, Tume hiyo itakuwa na jukumu la kupitia kwa kina masuala yote yanayohusu fidia, kubaini changamoto zilizopo, pamoja na kushauri Serikali juu ya hatua stahiki za kuchukua ili kuhakikisha haki inatendeka kwa wananchi wanaohusika.

