ZANZIBAR-Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mheshimiwa Dkt. Hussein Ali Mwinyi, ametuma salamu za rambirambi kwa Mheshimiwa Jude Thaddaeus Ruwa’ichi, OFMCap, Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu la Dar es Salaam, Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC), viongozi wa dini na waumini wote kufuatia kifo cha Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo, Askofu Mstaafu wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam.
Rais Dkt. Mwinyi amepokea kwa masikitiko makubwa taarifa za kifo hicho kilichotokea usiku wa Februari 19,2026 katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKIC) jijini Dar es Salaam.
Amesema,marehemu Kardinali Pengo atakumbukwa kwa mchango wake mkubwa katika kuliongoza Kanisa Katoliki kwa hekima, unyenyekevu na kujitolea, pamoja na juhudi zake za kuimarisha maadili, amani na mshikamano wa kitaifa.
Rais Dkt. Mwinyi amewaombea faraja na uvumilivu wote walioguswa na msiba huo, na kumuombea marehemu apumzike kwa amani.

