DODOMA-Serikali imetangaza kupunguza gharama za leseni na ada za maombi kwa wabunifu, watayarishaji wa maudhui na kwa Vijana wanaotumia majukwaa ya Mitandao ya Kijamii nchini Tanzania lengo likiwa ni kuwapunguzia gharama za uendeshaji, kuchochea ajira na kukuza mchango wa uchumi wa Kidijitali katika pato la Taifa.
Kauli hiyo imetolewa na Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Hamis Mwinjuma leo Alhamisi Februari 12, 2026 Mjini Dodoma kwenye Mkutano Mkuu wa mwaka wa Vyombo vya Utangazaji nchini, akisema hatua hiyo inafuatia ukusanyaji wa maoni kutoka kwa watengeneza maudhui walioeleza kuhusu gharama kubwa za leseni.
"Mapitio yamefanyiwa kazi na yameleta unafuu mkubwa ambapo sasa ada ya leseni imepunguzwa kwa kiwango kikubwa kutoka Shilingi 500,000 hadi 50,000 huku ada ya maombi ikiwa ni Shilingi 10,000 pekee. Vilevile kwa wakusanyaji wa maudhui mtandaoni ada ya leseni imepungua kutoka 1,000,000 hadi 100,000 na ada ya maombi ikiwa ni Shilingi 20,000 pekee,"amesema Mhe. Mwinjuma.
Kulingana na Naibu Waziri huyo, hatua hizo za serikali ni za kimkakati katika kuhamasiaha pia urasimishaji wwa shughuli za kidijitali, akisema ni imani ya serikali kuwa gharama hizo rafiki na jumuishi zitaongeza ushindani wenye tija, uwajibikaji na ubora wa maudhui ya mtandaoni.
Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) Dkt. Jabiri Kuwe Bakari amebainisha kuwa Mamlaka hiyo pia imeanza mchakato wa maandalizi ya utangazaji wa redio kwa njia ya Kidijitali kwa kuhuisha kanuni zilizokuwepo na kwamba utangazaji huo utaanza kwenye Mikoa ya Dar Es Salaam, Arusha, Mwanza, Mbeya na Mkoani Dodoma.
Tags
Breaking News
Habari
Leseni Maudhui
Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA)
Usajili Mitandaoni ya Kijamii
