GENEVA-Mganga Mkuu wa Serikali, Dkt. Grace Magembe, ametumia fursa ya mkutano wa 158 wa Bodi Tendaji ya Shirika la Afya Duniani (WHO) unaoendelea jijini Geneva Uswis kwa mikutano ya pembezoni kuelezea jitihada za nchi za uimarishaji wa huduma za afya.
Akiwa kwenye mkutano huo Februari 06, 2026, Dkt. Magembe amekutana na Mkurugenzi wa Programu wa Unitaid, Bwana Robert Matiru ambapo katika mazungumzo yao, Dkt. Magembe amesema mikakati na juhudi zinazotekelezwa na Serikali ya Tanzania, chini ya uongozi wa Waziri wa Afya, Mhe. Mohamed Mchengerwa) ikiwemo za kuweka mazingira wezeshi kwa wazalishaji wa bidhaa za afya.
"Tumetumia fursa hii kukutana na shirika hili leo kwa sababu linafanya kazi na makampuni mbalimbali duniani kwa kuyaunganisha na utaalamu, mabenki na fursa za mikopo nafuu ili kuyawezesha kuanzisha viwanda vya bidhaa za afya zenye ubora na ushindani wa kimataifa," amesema Dkt. Magembe
Kwa upande wake Mkurugenzi wa Programu wa Unitaid, Bwana Robert Matiru, amesema kuwa Unitaid inaendelea kushirikiana na Tanzania ili kuimarisha uwezo wa Mamlaka ya Dawa na Vifaa Tiba Tanzania (TMDA), ikiwemo kuwezesha kupandishwa daraja kutoka ngazi ya tatu kwenda ngazi ya juu zaidi.
Kikao hicho kiliazimia kuimarisha ushirikiano kati ya Tanzania na Unitaid, ambapo wadau wa Unitaid waliahidi kufika Tanzania kukutana na viongozi na wadau mbalimbali, kuendelea kutoa ushauri wa kitaalamu, na kuteua wawakilishi wa mawasiliano (focal persons) kutoka kila upande ili kuharakisha utekelezaji wa makubaliano.
