NA DIRAMAKINI
MAMLAKA ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) imetangaza kuendelea na utaratibu wa kutoa Tuzo Maalum kwa Waandishi wa Habari Bora wanaochangia kwa kiwango kikubwa katika kuhabarisha umma kuhusu sayansi ya hali ya hewa pamoja na shughuli na taarifa mbalimbali za mamlaka hiyo.
Hayo ni kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa leo na Kitengo cha Masoko na Uhusiano cha Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA).
Lengo la tuzo hizo ni kutambua na kuthamini mchango wa wanahabari katika kuelimisha jamii juu ya masuala ya hali ya hewa, pamoja na kuimarisha ushirikiano kati ya TMA na vyombo vya habari nchini.
TMA imeeleza kuwa,waandishi watakaoshinda tuzo hizo watapatikana baada ya kazi zao kufanyiwa uchambuzi wa kina na kamati maalum ya majaji.
Aidha,uchambuzi huo utahusisha taarifa zote za habari za hali ya hewa zitakazowasilishwa rasmi katika ofisi za TMA kupitia barua pepe za media@meteo.go.tz au mediahaliyayhewa@gmail.com.
Pia, mamlaka hiyo imesisitiza kuwa ni kazi zitakazotumwa kupitia barua pepe pekee ndizo zitakazozingatiwa, hatua inayolenga kuhakikisha uwazi, usawa na haki katika mchakato mzima wa upatikanaji wa mwandishi bora.
Taarifa zilizotajwa kushiriki katika tuzo hizo ni zile zitakazochapishwa au kurushwa hewani kuanzia Julai 2025 hadi Juni 2026. Wanahabari wote nchini wanahimizwa kuwasilisha kazi zao ndani ya kipindi hicho ili kushiriki katika mchakato wa ushindani.
Tags
Habari
Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA)
Tanzania Meteorological Agency (TMA)
Utabiri wa Hali ya Hewa Tanzania

.jpg)