ZANZIBAR-Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Alhaj Dkt. Hussein Ali Mwinyi, ameishukuru Serikali ya Oman kwa kuendelea kutoa misaada inayochangia maendeleo ya Zanzibar katika sekta mbalimbali ikiwemo elimu, utalii, utamaduni na uhifadhi wa urithi wa Mji Mkongwe.
Rais Dkt. Mwinyi ameyasema hayo leo Machi 10, 2026, aliposhiriki futari iliyoandaliwa na Balozi Mdogo wa Oman Zanzibar, Balozi Said Salim Al-Sinawiy, katika Hoteli ya Golden Tulip, Airport, Mkoa wa Mjini Magharibi.
Amesema, Oman imeendelea kuwa na uhusiano wa kihistoria na kidugu na Zanzibar na kuahidi kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itaendelea kuimarisha ushirikiano huo.
Kwa upande wake, Balozi Said Salim Al-Sinawiy amemhakikishia Rais Dkt. Mwinyi kuwa Oman itaendelea kuwa mshirika muhimu wa maendeleo ya Zanzibar, hususan katika sekta za utalii, elimu, uchumi wa buluu pamoja na utamaduni.






