ZANZIBAR-Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, ameushauri uongozi wa Kituo cha Tafiti za Kiuchumi, Kijamii na Uchambuzi wa Sera Zanzibar (ZRCP) kuandaa mikutano na mijadala na wadau ili kuwaelimisha umuhimu wa kutumia matokeo ya tafiti katika utekelezaji wa majukumu yao.
Rais Dkt.Mwinyi ameyasema hayo leo Machi 24, 2026, alipokutana na Mkurugenzi Mkuu wa kituo hicho,Juma Reli pamoja na ujumbe wake waliofika Ikulu, Zanzibar.
Aidha, amebainisha umuhimu wa kufanya maboresho katika mifumo ya usajili wa malipo ya kidijitali ili kuimarisha muda na uwazi, hususan katika sekta ya umma, na kushauri kuangaliwa upya kwa sera, sheria na kanuni katika eneo hilo.
Naye Mkurugenzi Mkuu wa Kituo cha Tafiti za Kiuchumi, Kijamii na Uchambuzi wa Sera Zanzibar (ZRCP),Juma Hassan Reli, ameunga mkono mapendekezo hayo na kueleza kuwa kituo hicho kipo tayari kushirikiana na Serikali katika kutoa tafiti.








