DAR-Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi amesema, Watanzania wataendelea kumkumbuka na kumuenzi marehemu William Vangimembe Lukuvi kwa mchango wake wa utumishi alioutoa katika nyadhifa za uongozi mbalimbali alizoshika wakati wa uhai wake nchini ikiwemo kutatua changamoto za migogoro ya ardhi.
Dkt.Mwinyi ameyasema hayo katika ibada ya kuaga mwili wa aliyekuwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu) na Mbunge wa Jimbo la Isimani, marehemu William Vangimembe Lukuvi, iliyofanyika katika Viwanja vya Karimjee, jijini Dar es Salaam leo Machi 28,2026.
Aidha, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan amewaongoza waombolezaji, wakiwemo viongozi mbalimbali wa kitaifa na wananchi, katika ibada hiyo ya kumuaga marehemu Lukuvi.
Vilevile, viongozi mbalimbali wa Serikali,vyama vya siasa, dini na vyombo vya ulinzi na usalama wameshiriki katika ibada hiyo.
Marehemu William Lukuvi amefariki dunia Machi 25, 2026 katika Hospitali ya Benjamin Mkapa, jijini Dodoma. Anatarajiwa kuzikwa tarehe 31 Machi 2026, kijijini kwao Idodi, Iringa Vijijini mkoani Iringa.










