DODOMA-Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), amekutana na kufanya mazungumzo na Mkuu wa Uendeshaji wa Taasisi ya Uwekezaji wa Miundombinu Afrika (Africa50), Bi. Tshepidi Moremong katika Ofisi za Wizara ya Fedha, Treasury Square jijini Dodoma.

Pamoja na mambo mengine, wamejadili namna ya kuimarisha ushirikiano wa kimkakati katika kukuza sekta za kiuchumi na kijamii ikiwemo nishati, gesi asilia, TEHAMA, usafiri, hifadhi ya mazingira na ujenzi wa miundombinu ya bandari na miradi mingine katika pande mbili za Muungano (Tanzania Bara na Zanzibar).
Mhe. Balozi Omar alimhakikishia Kiongozi huyo kwamba Serikali inathamini mchango wa Taasisi hiyo ya Africa50 katika nyanja mbalimbali zinazochangia kuimarisha uchumi wa nchi na watu wake.
Kwa upande wake Mkuu wa Uendeshaji wa Taasisi ya Uwekezaji wa Miundombinu Afrika (Africa50), Bi. Tshepidi Moremong, alisema Taasisi hiyo itaendelea kushirikiana na Tanzania katika maeneo yote muhimu ya uwekezaji wa miundombinu ili kuiwezesha nchi kuwa na ukuaji endelevu wa kiuchumi.
Mkutano huo pia ulihudhuriwa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha, Dkt. Natu El-maamry Mwamba, Kamishna Msaidizi, Idara ya Fedha za Nje, Bw. Robert Mtengule, Afisa Mwandamizi wa Taasisi ya Africa50, Bi. Cyndia Kipchumba Nguli na maafisa wengine wa Wizara ya Fedha.
Africa50 ni Taasisi ya Kifedha ya Kimataifa inayowekeza katika miundombinu baranı Afrika, ikiwa na lengo la kuziba pengo la ufadhili wa miradi, Taasisi ambayo ilianzishwa Mwaka 2015, ikiwa na Makao yake Makuu, Casablanca nchini Morocco.







