MOROGORO-Wizara ya Fedha imewakutanisha Maafisa wa Ununuzi na Ugavi wa Serikali, katika mafunzo ya muda mfupi kuhusu mikakati ya utekelezaji wa shughuli za mnyororo wa ugavi endelevu.
Mafunzo hayo yaliyoratibiwa na Idara ya Sera za Ununuzi wa Umma, inayosimamiwa na Kaimu Kamishna wa Idara hiyo, Bw. Alex Haraba, yanaendeshwa na Wataalamu kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na Chuo Kikuu cha Mzumbe katika ukumbi wa mikutano wa Dar to Dom mkoani Morogoro, kuanzia tarehe 2 hadi 5 Machi 2026.
Mafunzo hayo yanalenga kuongeza uwezo wa kitaalamu wa Maafisa wa Ununuzi na Ugavi wa Serikali katika kutumia mbinu na mikakati inayochangia utekelezaji wa mnyororo wa ugavi endelevu, kwa kuzingatia masharti ya Vifungu vya 5(2)(b) na 5(3)(c) vya Sheria ya Ununuzi wa Umma, Sura ya 410, vinavyoelekeza kuwa shughuli zote za ununuzi wa umma, ugavi na uondoshaji wa mali zifanyike kwa kuzingatia kanuni za uendelevu.
Mafunzo hayo yamewakutanisha Maafisa wa Ununuzi na Ugavi wa Serikali kutoka mikoa ya Kagera, Katavi, Kigoma, Ruvuma, Mbeya, Iringa na Dar es Salaam.




