DODOMA-Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali imepekuwa Mikataba 2,562 ya Kitaifa, Kikanda na Kimataifa katika kipindi cha kuanzia Julai 2025 hadi Machi 2026.
Hayo yamesemwa na Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Dkt.Juma Zuberi Homera wakati akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa Bajeti kwa Mwaka wa Fedha 2025/2026, Mpango wa Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara na Taasisi zilizoko chini ya Wizara kwa mwaka wa fedha 2026/2027, tarehe 24 Aprili, 2026 Bungeni, Jijini Dodoma.
Dkt.Homera amesema kuwa, upekuzi huo umeimarisha ulinzi wa maslahi ya Serikali, kupunguza hatari za hasara za kifedha, kuongeza uwajibikaji katika matumizi ya fedha za umma, na kuhakikisha miradi ya maendeleo inatekelezwa kwa kuzingatia sheria na mikataba yenye tija kwa Taifa.
“Mhe. Mwenyekiti vilevile, Ofisi ilikamilisha upekuzi wa Hati za Makubaliano (Memoranda of Understanding) 396,"amesema Dkt.Homera.
Aidha, Waziri wa Katiba na Sheria ameeleza kuwa Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali imesimamia mikataba 2,821 iliyosainiwa kati ya Serikali na wadau mbalimbali.
Pia Ofisi ilipokea maombi ya kuvunja mikataba saba (7) ambapo ilishauri mikataba mitano (5) ivunjwe kwa mujibu wa masharti ya mikataba husika na mikataba miwili (2) ilishauriwa isivunjwe badala yake utekelezaji uendelee kwa mujibu wa masharti ya mikataba.
Katika hatua nyingine, Dkt.Homera ameeleza kuwa,Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali imesimamia majadiliano ambayo yamewezesha kuhitimishwa nje ya Mahakama.
“Jumla ya migogoro na madai 143 imefanyiwa kazi ambapo kiasi kilichodaiwa kabla ya majadiliano ni Shilingi trilioni 2.83. Kufuatia majadiliano hayo kiasi kitakacholipwa ni shilingi trilioni 2.18, hivyo, Serikali imeokoa Shilingi bilioni 646.22,"amesema Dkt.Homera.
Sambamba na hilo, Dkt. Homera amesema kuwa Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali imesimamia majadiliano yaliyofanikisha kusainiwa kwa mikataba tisa (9) yenye jumla ya thamani ya Shilingi trilioni 7.48.
Waziri wa Katiba na Sheria amempongeza, Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa Utendaji kazi wake na ushirikiano anaoutoa kwa Wizara na Taasisi zake katika kusimamia Sheria nchini.
“Aidha, ninamshukuru sana Mhe. Hamza Saidi Johari (Mb.), Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa jinsi anavyonipa ushirikiano katika kutekeleza majukumu ya Wizara pamoja na uratibu na usimamizi wa Sekta ya Sheria kwa ujumla,"amesema Dkt. Homera.
Hotuba ya Bajeti na Mpango wa Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara na Taasisi zilizoko chini yake kwa mwaka wa fedha 2026/2027, imesomwa, kujadiliwa na kisha kupitishwa na Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Tags
Bunge la Bajeti
Bunge la Tanzania
Habari
Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali
Wizara ya Katiba na Sheria
