DAR-Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Bw. Emmanuel Tutuba, amekutana na kufanya mazungumzo na Mkurugenzi Mtendaji na Afisa Mtendaji Mkuu wa Benki ya NMB, Bi. Ruth Zaipuna, ambapo wamejadili mwelekeo wa kimkakati wa benki hiyo na mchango wake katika kuendeleza ukuaji na maendeleo ya sekta ya fedha nchini.
Katika mazungumzo hayo, Bi. Zaipuna alimweleza Gavana kuhusu matokeo ya utekelezaji wa Mpango Mkakati wa NMB wa mwaka 2021 hadi 2025, pamoja na hatua zilizofikiwa katika utekelezaji wa Mpango Mkakati mpya wa mwaka 2026–2030, ambao amesema umeanza vizuri.
Aidha, alieleza kuwa NMB inatarajia kufanya maboresho katika Mfumo Mkuu wa Huduma za Kibenki (Core Banking System), hatua inayolenga kuongeza ufanisi wa utendaji kazi na kuboresha utoaji wa huduma mbalimbali za kifedha kwa wananchi.
Mazungumzo hayo pia yalihusu uwekezaji wa kimkakati unaoendelea kufanywa na NMB, hususan katika maeneo ya teknolojia na mageuzi ya kidijitali, ambayo ni muhimu katika kuongeza ufanisi, ubunifu na upatikanaji wa huduma za kifedha.
Kikao hicho kilifanyika tarehe 20 Julai 2026 katika ofisi Ndogo za Makao Makuu ya Benki Kuu, jijini Dar es Salaam.






