Kitabu cha Falsafa ya Sheria ya Mama Samia kuwa rejea muhimu ya sheria nchini

DAR-Naibu Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Zainab Katimba, amesema Serikali ya awamu ya sita chini ya uongozi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, imeendelea kuimarisha misingi ya utawala wa sheria kupitia maboresho ya sera, sheria na mifumo mbalimbali ya utoaji haki, hatua zinazolenga kujenga Taifa lenye haki, amani na maendeleo endelevu.
Mhe. Katimba ametoa kauli hiyo Julai 10, 2026, wakati wa hafla ya uzinduzi wa kitabu cha Falsafa ya Sheria ya Mama Samia (Mama Samia Doctrine of Law) kilichozinduliwa na Makamu wa Pili wa Rais wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Mhe. Hemed Suleiman Abdulla,akimwakilisha Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Mungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba.

Naibu Waziri Katimba amesema kuwa, kitabu hicho kina mchango muhimu katika taaluma ya sheria na uongozi kwa kuwa maudhui yake yanaakisi uongozi wa Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan katika utekelezaji wa majukumu yake kwa kuzingatia misingi ya utawala wa sheria, haki, uwajibikaji na utawala bora.

Alisema, kitabu hicho ni rejea muhimu kwa wanataaluma, watafiti, wanafunzi wa sheria na viongozi, kwani kinaeleza kwa kina mchango wa uongozi unaozingatia sheria katika kuimarisha taasisi za Serikali, kukuza demokrasia na kuhakikisha wananchi wanapata haki kwa usawa bila ubaguzi.
Mhe. Katimba alisisitiza kuwa, utawala wa sheria ni msingi wa dola ya kidemokrasia na nguzo muhimu ya maendeleo ya Taifa. Alieleza kuwa Serikali imeendelea kuweka mazingira yanayokuza misingi hiyo kupitia marekebisho ya sheria, sera na mifumo ya utoaji haki ili kuhakikisha haki inapatikana kwa wakati na kwa usawa kwa wananchi wote.

Aidha, alibainisha kuwa Wizara ya Katiba na Sheria inaendelea kutekeleza wajibu wake wa kuhakikisha wananchi wanapata haki kwa wakati kwa kuimarisha huduma za msaada wa kisheria, utoaji wa elimu ya sheria pamoja na utekelezaji wa awamu ya pili ya Kampeni ya Msaada wa Kisheria ya Mama Samia na kuendelea kuziimarisha taasisi zinazosimamia mnyororo wa haki nchini.

Katimba amesema misingi ya utawala wa sheria haiishii katika vyombo vya utoaji haki pekee, bali inahitaji ushiriki wa wananchi, taasisi za umma na binafsi pamoja na wadau mbalimbali ili kujenga jamii inayozingatia haki, uwajibikaji, ushirikishwaji na utawala bora.
Wito umetolewa kwa wadau wa sekta ya sheria, taasisi za elimu ya juu, watafiti na wananchi kwa ujumla kukisoma kitabu hicho ili kupata uelewa mpana kuhusu nafasi ya utawala wa sheria katika kujenga Taifa lenye haki, amani, maridhiano na maendeleo jumuishi kwani mafanikio ya Taifa yanategemea uwepo wa mfumo imara wa sheria unaolinda haki za wananchi na kuhimiza maendeleo endelevu.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

Know matter how large or small your business is, advertising here