NA DIRAMAKINI
BENKI Kuu ya Tanzania (BoT) imetangaza kufungua mnada wa Hati Fungani ya Serikali ya miaka 25, Na. 695 Mnada Na. 3 unaotarajiwa kufanyika Agosti 5, 2026.
Kwa mujibu wa tangazo la BoT, hati hiyo itakomaa Februari 5, 2051 ikiwa na riba ya asilimia 13.25 kwa mwaka, huku malipo ya kuponi yakifanyika mara mbili kwa mwaka, kila Februari 5 na Agosti 5.
BoT imeeleza kuwa, riba limbikizi ni Shilingi 0.0363 kwa kila Shilingi 100, huku kiwango cha chini cha uwekezaji kikiwa Shilingi milioni moja (Sh1,000,000).
Aidha, hati hiyo inaruhusu ushiriki wa Watanzania wanaoishi nje ya nchi pamoja na wakazi wa nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) na Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC).
